DEMOKRASIA halali ni ile inayoheshimu na kujali haki na uhuru wa wachache kama inavyowapa wengi nafasi ya kuamua na kuendesha mambo ya serikali.
Wazee, wastaafi. wasiojiweza, vijana na watoto ni lazima walindwe dhidi ya wale wanaoweza kutumia udhaifu wao kuwakandamiza katika jambo hili au lile.
Iwe ni mwiko katika nchi inayokubali demokrasia kuruhusu wanajeshi au polisi kuelekeza mitutu ya bunduki zao dhidi ya wananchi eti kwa sababu tu wanadamana.
Tuirejee katiba na hata ikija katiba mpya haki ya kuandamana iwe ni haki inayotambulika na kuheshimiwa wakati wote angalau kwa kujua hii ndio njia pekee ya kupunguza presha ya watu wenye malalamiko au wasioridhika na maamuzi au hali fulani katika eneo fulani la nchi au jamii.
Ni lazima tukubali kuwa jeshi na polisi, kama vyombo, vyenye watoto, ndugu, jamaa wa Watanzania kamwe havipo kwa ajili ya kuwahujumu ndugu zao bali kuhakikisha haki inatendeka wakati wote. Jeshi na polisi katika Afrika lazima lijengwe katika misingi ambayo kwayo ni yule mwenye haki ndiye anayeipata na asiye na haki asistahili kupata haki isiyo yake.
Vyombo vyetu vya dola lazima visisimuliwe na muamko na mwamsho wa demokrasia na haki za binadamu. Na kama kuna jambo la kujivunia kwa majeshi yetu lazima jambo hilo liwe ni kutetea na kulinda demokrasia daima dawamu.
Yeyote aliye rafiki wa demokrasia atastahili kuwa rafiki yao; na yeyote aliye dhidi ya demokrasia atakuwa ni adui yao. Ndivyo inavyotakiwa, ndivyo inavyostahili kuwa.
Hatuwezi kuwatumia watu wetu katika vyombo vya dola kama vile ndondocha au misukule au midubwana ambayo haijali nani mwenye haki na nani asiye na haki katika kutekeleza majukumu na wajibu wao wa kulinda nchi na watu wake.
Katika Afrika kundi lolote liwe la raia au jeshi linalokiuka haki za binadamu kwa kuua, kubaka na kutesa watu hata iwe kwa sababu gani lazima litengwe na kuonekana ni kundi la waovu. Lazima tuwe na maadili ya kitafia
yatakayodhihirisha pamoja na mambo mengine jinsi gani Watanzania wanatakiwa waishi -iwe katika hali ya ustawi na amani au hali ya kukosa staha na migogoro ya ndani kwa ndani au vita na nchi za nje.
***
Subscribe to:
Post Comments (Atom)

No comments:
Post a Comment