MIFUMO yetu ya utawala imejengwa kwa namna ambayo kwamba baadhi ya viongozi katika nchi na pengine jamaa zao huonekana kuwa juu ya sheria.
Kwa maneno mengine, wao wakifanya kosa sawa na la mtu mwingine wanaweza wasikamatwe wala kushtakiwa. Hili sio jambo zuri. Kama tumezikubali sheria fulani kuwa ni zetu basi ni lazima bila kujali nafasi, wadhifa au uwezo mtu sheria ifanye kazi sawasawa.
Ni muhimu kuhakikisha kuwa vyombo kama vile polisi na mahakama haviachiwi fursa ya kuuza na kununua haki za watu. Hilo likifanyika utakuwa mwanzo wa mengi mabaya yatakayoiandama nchi yetu. Na hili Mungu alieepushilie mbali. Kwa hiyo tusikubali ukubwa, uroho, uchu na wivu wa wachache miongoni mwetu kutumia mianya inayojitokeza popote pale kuuza au kununua haki ya mtu na hasa katika wakati kama huu ambapo sasa ardhi Tanzania imeanza kuonekana kuwa ni mali!
Demokrasia ya kweli itakuwepo tu pale ambapo kila mahala patatawalia na utawala wa kisheria na sio kinyume cha hivyo.
Kiongozi mzuri sio yule anayejionesha kwa watu bali yule ambaye hata kama haonekani mambo anayoyafanya yanaonekana.
Mara nyingi yule mtu anayetka kuonekana sana, akiwashughulisha watu huku na huko na hasa masuala yake binafsi na yale ya wale wanaomhusu yanapokuwa mengi kamwe hawezi kuwa kiongozi mzuri.
Kubwa katika hili, hata hivyo, ni ile tabia ya wanasiasa kutaka kubadili sheria na katiba ya nchi sio kwa sababu ya maslahi ya wananchi bali kwa sababu watalinda vyeo na nafasi waliyonayo katika jamii. Hili ni lazima likemewe na kupigwa vita na watu na taasisi zozote katika nchi iliyodhamiria kujenga demokrasia ya kweli.
***
Sunday, June 15, 2008
Subscribe to:
Post Comments (Atom)

No comments:
Post a Comment