IMEKUWA ni tabia ya kawaida kwa vyama tawala kutoa upendeleo kwa wale wanachama wake na kusahau kabisa kuwa hakitawali tu wanachama wake bali pia na wale wa chama au vyama mbadala.
Hili katika demokrasia ya kweli libadiike. Maana lina madhara makubwa sana kutokana na kuwatenga watu wengi katika kutoa mchango wao kwa maendeleo ya kijamii, kisiasa, kiuchumi na kiteknolojia.
Kwa namna za ajabu inaelekea chama kinachoshinda huwa kinajua ni nani watu wake na nani sio watu wake. Na hapo biashara haramu ya huyu ni mwenzetu na huyu si mwenzetu ndipo inaanza. Ulikuwa na biashara nzuri sasa chama tawala na serikali yake itaiua. Ulikuwa huna chochote sasa chama tawala kwa kuwa ni mwenzao kitahakikisha kwa jino na ukucha unafanikiwa katika mambo yako. Swali, je, kweli hii ni biashara halali? Na kama sio, ikiendelea, itatupeleka wapi?
Ni dhahiri kuwa haiwezekani kuwachukulia wanasiasa wa vyama mbadala kama vile ni maadui na nchi hii ifanikiwe katika mambo yake. Ni lazima tujifunze kuwachukulia wanasiasa wa vyama mbadala kama wenzetu na washirika katika dau la maendeleo ya nchi zetu ili mambo yetu na nafasi zetu wenyewe ziendelee kuheshimika na kutabirika.
Kwa maneno ni muhimu kwa upinzani kutambulika kama pia nao ni viongozi wa taifa na wapewe heshima na haki zote viongozi wanazostahili kadri ya uwezo wa taifa hili.
Kila inapowezekana akili na ubunifu na uzuzi wa wanasiasa wa vyama mbadala visiachiliwe vipotee bure bali vidakwe na kutumika kupata ufumbuzi wa matatizo mbalimbali ya watu na nchi yao.
Sio siri kwamba maendeleo na ustawi wa nchi kama Uingereza na Marekani vinapatikana sio haba kwa kugonganisha akili na ubunifu wa wanasiasa tofauti na kwa serikali ya wakati wowote kutumia kile kilicho bora na sio lazima kile kilichotoka kwa mwanasiasa wao. Hakuna mifano mingi mizuri ya kuiga toka Marekani lakini huu ni mfano bora kuliko yoyote kutoka mahala pengine popote ulimwenguni kuuiga kwa ajili ya maendeleo ya nchi yetu na Afrika kwa ujumla.
Aghalabu katika nchi zilizokosa mwelekeo Afrika ni zile zinazowanunua wanawake na vijana ili watu hao watumike kufanya ghasia dhidi ya vyama mbadala. Tusiruhusu jambo hili kutokea. Badala yake tubuni njia za kuwashirikisha vijana wetu bila kujali chama wanachotokea kuweza kupambana na umasikini wetu katika mazingira ya utandawazi ambao wao wana mengi ya kupoteza kama watatumiwa vibaya na wanasiasa wa nchi zetu.
Mfano wa Zimbabwe, Kenya, Ethiopia na Misri ni mifano ya uahlifu wa kisiasa unaofanyika machoni mwa Afrika na dunia nzima na watu kushindwa kukemea wale wanaotaka kubaki madarakani kwa gharama zote hata kama watakayoacha nyuma ni majivu ya mamilioni ya watu wao. ***
Subscribe to:
Post Comments (Atom)

No comments:
Post a Comment