TANZANIA imejaliwa kuliko nchi nyingi Afrika isipokuwa labda Kenya ambao ni washindani wetu katika lugha ya Kiswahili.
Ninasema Tanzania imejaliwa kwa sababu ndio nchi inayoweza kama ikipenda kuwa na Redio ya Kiswahili Afrika, Televisheni ya Kiswahili Afrika, Tovuti Kuu ya Kiswahili Afrika na gazeti na jarida la Kiswahili kwa Afrika nzima.
Vyombo hivyo vikijengwa kwa mfano wa BBC, Deutsche Welle, Aljazeera na vyombo vinginevyo kwa kutumia Kiswahili na kuutanguliza mbele utamaduni wa Afrika tunaweza kufungua fursa nyingi za kujiendeleza na kujiajiri kwa vijana wetu hapa nyumbani.
Ni dhahiri taasisi mbalimbali za Kiswahili zitashirikiana na chombo hicho ili kuwafundisha wote wanaosikiliza au kutazama vyombo hivyo kujifunza Kiswahili. Hali kadhalika, pakiwa na michezo mizuri ya kuigiza ya Kiafrika basi Afrika nzima kila jioni itakuwa inaketi kutazama kinachozalishwa na vijana wa Kitanzania.
Lakini kubwa zaidi ni kuwa vyombo hivyo vya habari vitachangia si haba katika kuharakisha kupatikana kwa umoja wa Afrika ambao sasa hivi tunatapatapa na hatujui njia ya kuuleta kwa upole na ustaarabu.
Ili tufikie hatua hiyo, hata hivyo, lazima vyombo vyote vya habari viwe vinavyomilikiwa na serikali, vyama vya kisiasa au vya watu binafsi lazima viwe huru kuendesha mambo yao bila kuvunja misingi na taratibu vyombo vya habari vilivyojiwekea.
***
Subscribe to:
Post Comments (Atom)

No comments:
Post a Comment