MAMBO yaliyotokea Arusha na Mwanza hivi karibuni, hususan kuhusiana na suala la nani aongoze halmashauri za miji hiyo limeanza kuzua wasiwasi kama viongozi wa CCM wana nia ya kweli ya kushirikiana na wananchi wengine ili kuipatia nchi hii katiba mpya na kuivusha Tanzania kuelekea kwenye demokraia isiyo na mizengwe, pana na ya kina mapema iwezekanavyo.
Inaonekama kama vile hivi sasa CCM haina mwenyewe; haijiamini; haijui inafanya nini na imeamua kutumia vibaya vyombo vya dola na serikali yake huku ikikiuka katiba iliyoko kushoto na kulia bila kujali wala kuogopa. Ubabe na maguvu haya yanayotumika bila kuwepo na sababu ya kuridhisha, yanakuja wakati tayari kuna malalamiko ya msingi dhidi ya chama hicho kutokana na jinsi uchaguzi mkuu ulivyoendeshwa mwaka jana.
Matukio haya yanawafanya baadhi ya watu pia kuamini kuwa CCM inadhani ina mkataba wa milele wa kuwatawala Watanzania; inalea ukabila wa kichama ambao ni mbaya kuliko ule wa kikakabila halisi; inajenga chuki kutoka kwa wananchi walio wengi; na inaonesha kama ni chama chenye uchu na uroho wa kutisha na iko tayari kufanya lolote ili kubaki madarkani. Na baya zaidi ni kuwa chama hicho kinashindwa kujifunza kutoka kwingineko Afrika, Marekani ya Kusini na Iliyoko Urussi ya zamani, pengine kwa kuwa sasa ni muflisi wa wanaitikadi na viongozi wanaofaa kukabiliana na changamoto na hali ya kisiasa inayokikabili chama hicho hivi leo.
Ni kutokana na hofu hii ndiyo maana nimeonelea leo kusaidia nchi yetu kwa kukishajiisha chama cha mapinduzi kufungua macho yake katika mambo kadhaa ili kuepusha shari kubwa inayoweza kutokea baadaye. Watanzania wa leo sio wajinga wa enzi za ujamaa na kujitegemea, bali werevu waliofunguliwa macho na umaskini, njaa ya raha na furaha, kiu ya haki na usawa, ufisadi, rushwa na madhambi mengine ambayo yameendelea kukua dhidi ya kelele za siasa za mambo kuwa kinyume cha hivyo.
Ninaamini bado CCM kinaweza kuwa chama imara na madhubuti bila ya uoga, ujanja, nabavu na ubabe kwa kujenga haki na usawa wa kisiasa nchini. Kinyume cha hivyo, chama hicho kitakuwa kinatengeneza mazingira magumu na mabaya kwa chama hicho na nchi yetu katika chaguzi zijazo.
Ukikiimarisha Chama cha Mapinduzi (CCM) kiutawala, kikatiba, kisheria, kihaki, kiusawa, kiuongozi na kidemokrasia utakuwa pia unaviimarisha vyama mbadala na nchi kwa ujumla. Amani na umoja unaoimbwa kila siku vitapatikana na sio kwa kufanya mambo kinyume cha hivyo.
Kama tunavyoingia mwaka 2011 na mchakato wa Katiba Mpya ya nchi upo umuhimu pia kwa Chama Tawala nacho kupitia kwa makini katiba yake. Katika kupitia huko chama hicho kiangalie masuala ya muundo, mifumo, utawala, usimamizi, uongozi na udhibiti wa shughuli zake kwa nia ya kukiwezesha kuaminiwa, kujihalalisha, kuwajibika, ufanisi na ufanifu zaidi.
Nguvu za chama hicho kwa kiasi kikubwa zinatokana na kuwa na mtandao nchi nzima. Mtandao huo unaanizia kwanye matawi/mashina, mtaa, kata, tarafa, wilaya, mkoa hadi taifa. Tatizo kubwa ninaloliona kwa sasa ni mitihani na changamoto za uratibu, usimamizi, udhibiti na ukaguzi wa shughuli za chama katika ngazi mbalimbali.
Ni vyema chama kiangalie kama muundo wake na mifumo yake ya kazi hivi leo unaendana na changamoto hizo hapo juu kwa nia ya kuwafanya watendaji wake kuwajibika ipasavyo kwa wanachama na wananchi. Hali kadhalika kuhakikisha kuwa vyombo vya dola vinatumikia Watanzania wote bila kujali mtu ana itikadi gani au ni wa chama gani. Kikatiba iwe ni kosa kuchanganisha mambo na kazi za chama hicho na yale ya serikali. Hivi ni vitu viwli tofauti na iwe hivyo. Serikali inastahili kuwepo wakati wote, lakini chama kinaweza kuondolewa madarakani au hata kufa kikikosa ridhaa ya wananchi.
Muhimu pia ni kwa chama kutenganisha dhahiri bin shayiri mipaka yake ya kiuongozi na serikali. Isifikie mahala pa chama chochote kupora mamlaka ya mangimeza au watumishi wa serikali na hivyo kuhatarisha dhana ya serikali endelevu katika mabadiliko ya viongozi kidemokrasia katika vipindi bayana. Yaani polisi, mahakimu, wanajeshi na watumishi wote wa serikali wasiwe na wasiwasi chama fulani kinapoondolewa madarakani na chama kingine kuingia madarakani. Ni lazima sikuzote watumishi wa serikali wawe juu ya chama chochote cha kisiasa katika tarafu zao na sio kinyume cha hili. Watumishi wa serikali kukubali kuporwa madaraka na wanasiasa ndiko kulikotufikisha hapa tulipo leo. Enzi za chama kushika utamu bado zipo, laki si za chama kushika hatamu!
Changamoto nyingine inakuja kwenye suala la wale wanaopewa dhamana ya kukiongoza chama hicho katika ngazi mbalimbali. Hivi sasa kuna madai ya ukabila wa kichama. Na ndio maana kuna wana CCM wanaamini wao wana haki zaidi ya kuchaguliwa kuiko wenzao kwa upande mmoja, na kwa upande mwingine CCM haitaki na haifikirii hapa bara kuwashirikisha wanachama wa vyama vingine katika kuongoza nchi yao. Na kama alivyosema baba wa taifa ukianzisha mgwanyiko kati ya watu kwa nia au shabaha yoyote ile mgawanyiko hauishii pale ulipokusudia. Jambo hilo haliwezi kuwa chanya bali hafi. Mgawanyiko mmoja huzaa mgawanyiko mwingine. Kichama ni kwamba ukiwa na nchi ambayo viongozi wake ni wa kabila la chama na viongozi wengine wote wa serikali (sio chama) hawakubaliki kutoka chama kingine unakuwa ni mwanzo sasa wa wanachama wenyewe kugawanyika kati ya wanachama viongozi na wanachama wafuasi. Na katika wanachama viongozi hugawanyika kati ya viongozi wetu na viongozi wao. Na kati ya viongozi wetu hugawanyika tena kati ya wateule na wasiokuwa wateule. Matokeo ya hili ni kukisambaratisha chama kwa kukosa gundi ndani na nje ya chama katika kukiunganisha.
Chama lazima kichague viongozi wenye elimu, ujuzi, uzoefu, tija, hulka na saikolojia taibu na sifa nyingine zinazotakiwa katika kufanikisha nafasi mtu anayopewa. Isitokee kumchagua mtu tu kwa sababu ni mwanachama na kisha mtu huyo akawa ni mzigo na tatizo kwa chama na viongozi wake.
Sielewi ni kwa kiasi gani chama hiki kina Sera na Mifumo ya Menejimenti ya Rasilimali Watu bora na inayofanya kazi. Ila tatizo moja ninaloliona ni la ajira, mishahara na malipo mengineyo. Bila ya kuwa na mifumo ya ajira na ujira sahihi chama hakiwezi kudhibiti masuala yake mengine ya uhai na kimaendeleo.
Katika miaka hii ya leo kukosa sera nzuri ya rasilimali watu (Human Resource Management) ni kukaribisha uongozi dhaifu kielimu, kimaarifa na kiulimwengu katika safu za uongozi wa chama na zile za utumishi wa umma kwa ujumla. Jambo litakoloongeza tatizo la ukabila wa kichama na kushindwa kudhibiti mapato ya chama,
mali za chama na miradi ya chama. Hali inayolea ubabe wa viongozi ngazi za chini, rushwa, kulindana na kukidhoofisha chama katika ngazi hiyo.
Wakati waasisi wa chama walikuwa na nia nzuri ya kukifanya chama kijiendeshe chenyewe lakini ukweli ni kwamba
kimeshindwa kujiendesha kiuchumi na kifedha. Na habari za hivi karibuni ni kwamba chama kiko katika hali mbaya. Kwa kuwa kimekosa mifumo ya ndani ya kiujasirimali, kiutafutaji na uzalishaji kipato chama hicho kimekuwa kikitegemea watu binafsi kukifundisha ujanja wa kupata fedha na mara nyingi kukiingiza mkenge.
Ni hatari kubwa mno kwa chama kumtegemea mtu mmoja au wawili kukitafutia mapato, maana upo uwezekano mkubwa wa chama hicho kuuzwa bila kujua kinachoendelea. Lazima muundo na mifumo ya chama ukiwezeshe kuzalisha pato la kukidhi gharama zake za kila mwaka na sio vinginevyo. Hili hakika ndilo linaloonesha uhai wa chama, vinginevyo unakuwa na chama kinachoishi kwa kutegemea hewa ya oksijeni ya kupuliziwa na wazuri na wabaya wake.
Chama sio mapato tu ni pamoja na kuwa na mameneja, wajasirimali wa ndani na wana itikadi wanaoendana na wakati na wanaosaidiana kukipatia chama mikakati-mipango inayofanya kazi.
Ni muhimu pia CCM iangalie ubora na udhaifu wa kuwa na wakuu wa mikoa na wilaya wasiochaguliwa na wananchi au wanaochaguliwa na wananchi. Uamuzi wa kuwa na mikoa-huru kiuchumi na kijamii ambayo bado CCM ina sauti utakuwa ni wa faida kwa chama hicho bila ya kusubiri mabadiliko ya katiba yatakayodai jambo hili likiwa na chagizo la chama kinachoshinda kura katika mkoa fulani kuwa ndicho kinachoendesha pia serikali ya mkoa husika.
Kuna wanaosema CCM imeifanya Tanzania kuwa na nchi-nyanya (nanny state). Kwa maana ya kwamba serikali yake inavumilia wanaofanya makosa ili mradi tu wanakiunga chama mkono. Aidha, sheria nyingi hupuuzwa na hakuna kinachofanyika ili mradi wanaovunja sheria hawaungi mkono upinzani bali wanakiunga mkono chama tawala. Bila ya utawala wa kisheria iwe kwa viongozi au wananchi itakuwa ni kazi sana kuwa na chama bora nchini.
Katika dunia hii ambayo baadhi ya wezi na wahalifu wengine hujitahidi kufaulu ushindani na mitihani yake ili awe polisi, hakimu au mwanasheria sio kwa nia ya kulinda watu bali kurahisisha maslahi yake binafsi; Ni katika dunia hii ambayo mzinzi mzoefu hujitahidi kuwa padri au shehe ili ufanyaji madhambi wake usiwe rahisi kujulikana ni muhimu kwa chama makini kuwaangalia wale inayowapa kazi ya kukijenga na kukiendeleza. Ili wasijikute wana wabomoaji wengi zaidi kuliko ya wajenzi. Iwe ndani ya chama au ndani ya serikali.
Katika tafiti binafsi, nimegundua kuwa mengi ya matatizo ambayo nchi yetu leo inapitia yanasababishwa na vyama vya kisiasa, ikiwemo chama tawala kukosa njia za uhakika na zinazojulikana za kupata mapato ya kujiendesha na yale ya kugharamia kampeni wakati wa uchaguzi. Bila ya tatizo hili kutafutiwa dawa itakuwa ni ndoto iwe kwa chama kilicho madarakani au kwa kitakachokuja au vitakavyokuja baadaye kuepuka balaa la rushwa, ufisadi, wizi, dhuluma na uonevu usio na sababu wa wananchi wasio na hatia zaidi ya kuunga mkono chama wanachoona kina misingi ya haki na usawa zaidi kuliko ya kile kinachotawala kwa wakati huo .
Inasikitisha kuona kuwa kuna waandishi, watangazaji na wanahabari, viongozi wa dini na watu wengine ambao kwa sababu moja au nyingine wanaamua kuona huku wamevaa miwani ya watu wanaoona karibu lakini hawaoni ya mbali. Huu ni msiba mkubwa. Na hasa pale kitendo cha kuvunja sheria kinapofanywa na watumishi wa chama tawala. Ni watu kama hawa ambao hawana tofauti kabisa na watu wa Radio Mille Colonnes ya Rwanda na kile ilichokisababishia nchi hiyo. Haiwezekani ikawa siku zote kuwa chama tawala na viongozi wake ndio watu wasiofanya makosa, lakini watu wengine sikuzote ndiyo wenye hatia. Wanaokataa kuona ukweli kwa kuwa wanaajiriwa na serikali au chama fulani ni mamluki na mkosi kwa Watanzania. Ndio wanaosababisha matatizo kama tunayoyaona katika nchi nyingine za Kiafrika. Na watu kama hawa wajue ni waliolaaniwa jana, leo na kesho pia. Hii ni laana ya kizazi cha kwanza hadi kizazi cha mwisho. Kweli, watanufaika kwa posho na hongo za chama hicho lakini kizazi chao chote kitakuwa kizazi kilicholaaniwa na kitakachokuwa kikiadhibiwa hapa hapa duniani kwa kuingiza nchi na watu katika matatizo, wakati walikuwa na nafasi ya kuikoa nchi.
Swali wengi wanalojiuliza ni kama viongozi na polisi mkoani Arusha wanafahamu mkoa wanaoishi au wote ni watu wa kuja. Maana Arusha ni kitovu cha Utalii Tanzania kama sio Afrika Mashariki. Kitendo walichokifanya kimeonekana 'laivu' dunia nzima. Hii leo picha iliyotoka Arusha ni kwamba nchi iko matatani, haikaliki na haifai kutembelewa na watalii. Je, haya ndiyo waliyoyataka. Hivi kwa kutumia akili zao kweli walishindwa kuwalinda na kudhibiti walioandamana toka mwanzo mpaka mwisho. Au wao kama kawaida yao walikuwa wakitekeleza amri toka juu. Hii, haithibitishi tukiwachia wanasiasa kututawala toka Dar es salaam mwishowe watatuingiza kwenye matatizo yasiyokwisha. Na kwamba wakati umefika wa mikoa kama ilivyo Zanzibar kujitawala yenyewe ?
Watanzania wenzangu tusiwaachie watu tuliowaajiri kutuongoza kufikia mahala ambapo inakuwa ni sawa na wezi kumwamuru mbwa wao kumng'ata mtu anayeibiwa na sisi tukaona kila kitu ni sawa tu.
Hivi polisi anayejua wajibu wake kwa umma anaweza akakubali kuamrishwa toka juu na kwenda bila fikira au roho kufanya kazi zake. Wewe ukiambiwa ua watu wako uue tu, bila kuangalia kama amri kama hiyo na mazingira yaliyopo unastahili kufanya unyama huo. Je, unaweza kweli kugeuzia baba, mama na ndugu zako bunduki na risasi za moto wakati wao wanafanya maandamano bila silaha.
Hivi jamaa hawa wanajua kuwa katiba ya nchi inamruhusu mtu kuandamana wakati wowote, mahala popote na kazi ya polisi ni kutoa ulinzi kwa raia wanaoandamana na sio kuwatupia risasi za moto.
Je, wana uwezo wa kufikiri kuwa amri au sheria yoyote inayokinzana na katiba ambayo ni sheria mama ni kitu au amri batili na haramu?
Itambulike kwamba, 'Mbuyu unapokaribia kuanguka ndio kwanza huwa unavimba na kujitanua kwa ukubwa na maguvu,' na kila dalili kwa baadhi ya wanasiasa zimeanza kuonekana likiendana na hili. Kadri watu waadilifu wanavyowahamasisha wananchi kukataa dhuluma, uonevu, wizi, ufisadi ndivyo pia 'wafa maji' watakavyozidi kuwang'ang'ania watu wema ili kufa nao. Hawa tena sio watu wa kuwashika mikono bali ni watu wa kuwapa fimbo au magogo wajiokoe wenyewe.
Somo kwa Watanzania hivi leo ni kuwa wasipoangalia wataendelea kutawaliwa na watu wanaotumia ghiliba, wizi, ubabe, kupandisha bei ovyo baada ya kuingia kwenye mikataba ya kipumbavu, dhuluma na uonevu wakati kuna vyama mbadala vyenye tabia tofauti na vitakavyowaletea nafuu kubwa katika maisha yao ya kila siku.
Uoga ni tabia ya kawaida kwa watawala ambao wameshindwa kuleta mabadiliko ya kimsingi kwa watu wanaowaongoza. Lakini wananchi kuwa waoga kukataa uonevu, dhuluma, wizi na ubaya mwingine ni kitendo cha aibu, dharau na 'kike' ambacho hata dini zinazojulikana huwa hazikubali. Ndiyo hali ya CCM sasa hivi na makombora inayotupa ovyo kwa wananchi wasio na hatia na kusingizia lawama kwingine.
Chama chochote cha kisiasa kitaendelea kuwa madarakani sio kwa ubabe, maguvu na kutumia vyombo vya dola kukandamiza watu wengine. Kubakia huko kutawezekana tu ikiwa chama hicho kina ridhaa ya wananchi. Chama kikiisha anza kupoteza ridhaa ya wananchi ujanja sio kutumia ulaghai na ubabe bali kujisahihisha, kujirekebisha na kujizaa upya ili kuukabili ukweli na hali halisi iliyopo ana kwa ana na sio vinginevyo.
Waandishi na wananchi wengine wasikubali kuwa vipofu kwa yale yaliyojiri Arusha na Mwanza kwa vitisho kwamba watu wakipigania haki zao basi watakuwa wanavunja sheria. Mida ya kukubali sheria za kimabavu na kibabe siku zote zinahesabiwa. Na ndio maana upo umuhimu wa kuwa na Tume Huru ya Uandaaji wa Katiba Mpya na sio Tume itakayoendeshwa kwa rimoti kontroli kutoka Bagamoyo.
CCM ikiendelea kuzuia na kuwakatalia watu haki zao za kikatiba kwa kutumia watu wasioijua katiba na haki za wananchi wengine ni dhahiri na wananchi nao WATAENDELEA KUKIKATAA CHAMA CHA MAPINDUZI !
Mzimu wa Mwalimu utaendelea kuwaonesha na kuwadhihirishia pamoja na jitihada zao za kukipaka udini chama cha CHADEMA, bado chama hicho ndicho kimbilio la kufaa kwa Watanzania na sio vinginevyo.
Kila CCM ikitumia vyombo vya dola kulemaza na hata kuua watu basi musuli na vifua vya wananchi wasiokubali dhuluma vitazidi kupanuka na kugeuka chuma kwa mapambano ambayo chama hicho kikiwa kistraarabu na kinachowajali Watanzania kinaweza kuwaepusha.
Kila CCM ikishindwa kubadili hali ya wananchi na kuwaacha katika unyonge na umaskini wa kutisha, ijue hili litazidi kuvipa nguvu vyamba mbadala nchini.
Kila CCM ikiivunja kwa mabavu na kiburi katiba yake iliyopo ndivyo pia madai na misukumo ya raia kutaka katiba mpya itakayoandaliwa na watu huru na kasoro na maradhi ya CCM ndivyo yatakavyozidi kurindima.
Jinsi CCM inavyoua na kulemaza watu wasio na hatia kwa kutumia polisi wake ndivyo pia vijana wapenda haki wanavyozidi kuikataa na ndvyo pia wanavyozaliwa watoto watakaokichukia chama hicho milele.
Yaliyojiri Arusha na Mwanza na yanayoendelea kwingineko kwa jitihada za CCM kubaki madarakani kwa hila, ulaghai, wizi na mabadu; sio tu ni uthibitisho tosha kuwa tumechelewa kuipata katiba mpya bali pia bado kuna Watanzania wanaotishia kuikataa demokrasia pale wao wanapogeuka kuwa watu walioshindwa. Aidha, tumeshuhudia dhahiri kuwa watakaovunja amani na umoja wa nchi hii sio wengine ila wale watakaothubutu kutumia polisi na vyombo vya dola vibaya kwa faida zao binafsi na sio maslahi ya nchi hii!
Na mojawapo ya kazi ya katiba hiyo mpya iwe ni kukomesha kabisa vyombo vya dola kutumiwa na wanasiasa; ubomojaji wa nchi kwa mikataba ya kiwizi; ulaghai na wizi wa haki za watu unaofanywa na vyama vya kisiasa; na viongozi bomu wanaong'ang'ania kubaki kwenye vyeo, lakini hawawezi kuongoza wala kujenga nchi.
Saturday, January 8, 2011
Subscribe to:
Posts (Atom)
