Sunday, July 26, 2009

DEMOKRASIA, TEKNOHAMA NA WIZI WA KURA

INDIA, taifa lenye kufuata demokrasia na lenye watu wengi kuliko mataifa mengine duniani yanayofuata demokrasia mwaka huu kwa mara ya kwanza liliweza kuendesha uchaguzi wake mkuu kwa kutumia TEKNOHAMA.

Nchi hiyo imedhihrisha inawezekana kabisa kuondoa mkono wa mtu unaolaumiwa sana kwa kupandikiza majina ya uongo katika daftari la wapiga kura, kutowaandikisha wapiga kura walio na haki ya kupiga kura, kuingiza kura za uongo, kuharibu na kupoteza kura za halali na mambo mengine kama hayo.

Jambo hili linaashiria kwamba ikiwa patakuwa na muundo na mfumo unaokubalika wa Katiba mpya katika mfumo wa vyama vingi na Tume Huru isiyoegemea upande mmoja na kisha kutumiwa TEKNOHAMA haki na usawa katika upigaji kura ni mambo yanayoweza kuwa kitu cha uhakika zaidi kuliko ilivyo sasa.

Katika nchi nyingi za Kiafrika kile kinachoitwa Tume ya Uchaguzi ni kiumbe cha chama tawala na seriklai yake. Ni zao la Katiba za viraka na ziizopitwa na wakati. Ni zao za sheria zilizopitwa na wakati na zisizokidhi matarajio ya ushindani wa kisiasa, soko huru na haki za binadamu.

Kwa kuwa wanaoongoza taasisi hizo ni watu wanaolishwa fadhila na chama tawala matokeo yake sikuzote ni kukisaidia na kukipendelea chama hicho kishinde hata pale kinapostahili kushindwa.

Uhakika wa kura ya mpiga kura kwenda kwa yule anayemtaka, Haki na Ukweli ni vitu vinavyowezekana endapo kutakuwa na upigaji kura kieletroniki.

Madhali nchi kama India imeshaanza kazi kama hii kinachotakiwa ni kwa chombo cha Umoja wa Mataifa kinachoshughulika na Demokrasia na Haki za Binadamu kuwa wakala wa kukodisha vifaa vya Teknohama toka India ili vitumike wakati wa uchaguzi katika nchi mbalimbali za Kiafrika na dunia ya tatu kwa ujumla.

Vinginevyo, utafiti uendelee kufanyika zaidi ili kuja na mashine bora zaidi za kieletroniki zitakazoondoa kabisa wizi na ujanja wa aina nyingine wakati wa kupiga kura Afrika na duniani kote kwa ujumla.

Ikumbukwe kwamba WIZI NA RUSHWA KUBWA KULIKO ZOTE ni zile zinatokea wakati wa chaguzi katika nchi mbalimbali Afrika. Ukkomesha wizi na rushwa hii katika ngazi hiyo utakuwa umelisaidia bara hili sio haba.

Nini kifanyike
Serikali ya India ambayo kwa sasa iko karibu na nchi za Kiafrika kuliko wakati wowote uko nyuma inaweza kuanza kwa kuwaalika wanasiasa na vijana wa vyama mbalimbali vya kisiasa kwenda India ili kupata mafunzo ya muda mfupi kuhusu upigaji kura kielektroniki. Huko watajifunza kwa nadharia na vitendo na hivyo kutambua uboa na udhaifu wa njia hiyo ya kupiga kura. Endapo wataona ni jambo linaloifaa Tanzania basi bila shaka watakuwa na hamasa ya kuja kulieleza, kulieneza na kulifanya likubalike hapa Afrika kwa urahisi.

Kama shabiki wa Teknohama nimekuwa nikijiuliza hivi kuna uwezekano wa kuwa na sanduku la kura lenye kutumia betri na linaloweza sio tu kupokea kura bali kuhakikisha halikubali kura mbaya na kisha kupiga hesabu ndani kwa ndani na kuonesha kwenye skrini juu yake kila mgombea kapata kura ngapi? Kisha boksi hilo liwe na uwezo wa kutuma majibu hayo kioto kwenda kwenye kompyuta kuu ya uchaguzi kiwilaya, kimkoa na kitaifa ?

Boksi hilo litakuwa na uwezo pia wa kuainisha vidole vya mpiga kura na kama namba yake inaendana na alama hiyo anakubalika na kama sivyo anakataliwa?

Simu za Mkononi
Kuna wanaofikiria pia upo uwezekano wa kutumia simu za mkononi maalum au za kawaida katika uchaguzi mkuu na upigaji kura wakati wowote.

Simu maalum za kupiga kura zitakuwa ni simu ambazo zinatumika kwa ajili hiyo tu na taifa litawajibika kumnunulia kila mpigaji kura simu yake kutokana na kodi za wananchi. Simu hiyo itanunuliwa mara moja tu katika maisha ya mtu. Na wale wanaokufa zitarekebishwa ili wapewe wapigaji kura wapya wanaoingia kwenye orodha ya wapiga kura baada ya kutimiza umri wao.

Aidha kwa simu za kawaida baada ya wananchi kuandikisha simu zao zote itachaguliwa namba moja mama itakayokubalika katika kupiga kura na masuala mengine ya kijamii na kiuchumi katika mfumo maalum wa kurahisisha na kupanua matumizi ya simu za mkononi.

Kwa kutumia namba ya simu yako iliyoandikishwa na inayokubalika baada ya kila kitu kuthibitishwa utaweza kupiga kura yako ukiwa unastarehe nyumbani kwako bila ya kwenda mahala ukacheleweshwa, kunyeshewa na mvua na kuchomwa na jua bila ya sababu ya maana. Jambo hili sio tu litawapa nafuu kubwa wapiga kura lakini pia litachangia idadi kubwa ya watu kupiga kura wakati wowote upigaji kura unapohitajika bila ya kugonja miaka mitano.

Itakuwa ni rahisi pia kufanya chaguzi ndogo kwa sababu gharama yake itakuwa ni ile tu ya uratibu na mawasiliano.

Kwa kifupi, Waafrika ambao ndio wanaokabiliwa na tatizo hili la wizi wa kura wanastahili kuwa mstari wa mbele kutafuta ufumbuzi wake. Mawazo haya ninaamini yanaweza yasifae au kukubalika lakini lengo langu la kuamsha mjadala kama Teknohama inaweza kutusaidia kuwa na chaguzi za huru, haki na zenye ukweli zaidi litakuwa limefanikiwa.

DEMOKRASIA NA TAASISI ZA KIJAMII NA KIIMANI

MWAKA 1961 Tanzania ilipopata uhuru kulikuwa na vikundi huru kadhaa vikishughulika na mambo mbalimbali kuanzia maslahi ya ukoo, mtaa na kabila. Taasisi nyingi zilizokuwepo zilikuwa kwa ajili ya kutoa huduma na msaada kwa makundi fulani ya kikabila, kieneo, kidini, kibiashara,kikazi na kiuzalishaji mali.

Miaka michache baadaye chama cha TANU kikaitangaza nchi hi ni ya chama kimoja. Makundi mengi ya kijamii na kiuchumi yakanyimwa haki na uhuru wa kufanya kazi zao za kuisaidia jamii au wanasiasa wakaingizwa kwenye makundi hayo ambao badala ya kujenga walivibomoa na kuvimalizia mbali kabisa.

Mbadala ukawa ni chama cha TANU na baadaye CCM kulazimisha watu wote waliotaka maendeleo na neema kujiunga na makundi maalum yaliyoanzishwa kwa nia, sababu na maguvu ya kukifanya chama hicho kiwe na nguvu na uwezo kuliko sehemu yoyote ya jamii katika nchi hii.

Makundi hayo ni pamoja na yale ya vijana,wanawake, wazee/wazazi, wafanyakazi, wanafunzi na kadhalika. Huu ukawa mwanzo wa kile ambacho leo tunaita ubaguzi wa kichama au kisiasa ambao ni ile hali ya chama tawala kutumia mabavu ili kujinufaisha na kuwanufaisha wale wanaokiunga mkono katika masuala mbalimbali ya kijamii, kiuchumi, kisiasa na kiutamaduni. Wengi watakumbuka kwamba ili mtu kuwa na uhakika wa kupata fursa ya kuendelea na masomo ulipaswa uwe na kadi ya TANU/CCM au vinginevyo ulikuwa huna njia nyingine ya kujiendeleza. Hili limekwisha kiuwaziwazi lakini bado liko kimafichomaficho.

Demokrasia ya kweli na inayofanya kazi haiwezi kuwepo kama kuna chama chochote cha siasa kinachotumia fursa ya kuwa chama kinachosimamia serikali kisha kuviamuru vyombo vya dola kubeza, kudharau, kupiga vita, kuvinyonya na kuvitendea isivyo haki vikundi vya kijamii visivyo na unasaba na chama tawala na jumuiya zake.

Ni muhimu kwa vijana, wanafunzi, wanawake, wazee, wafanyakazi, wanavijijini, wakulima, wafanyabiashara, watumishi wa umma na wengineo wawe na haki ya kuunda, kuanzisha na kuendeleza kikundi chochote cha kijamii na kiuchumi ambacho wanaamini kitakuwa na manufaa kwao na kwa jamaa zao na kwa jamii yao mtaani au kijijini.

Isipokuwa hivyo basi kutakuwa na mifukuto na migogoro na mioto ya chini kwa chini isiyoisha katika makundi ya kijamii ambayo badala ya kuchangia maendeleo ya watu vitakuwa ni vitu vinavyohujumu na kupoteza fursa mbalimbali za maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Mathalani, katiba inaruhusu haki ya kila mtu kuwa na uhuru wa kiimani na kuabudu. Kwa mapana yake na marefu ni kwamba raia yeyote wa nchi hii ana haki ya kukataa au kukubali kujiunga na kundi hili au lile katika masuala ya imani, dini na ibada. Na ni mwiko kwa serikali yoyote, iliyopo madarakani na zitakazokuja kupora na kupoka haki ya dini yoyote ile katika kukubali au kukataa taasisi fulani. Ni haki ya kidemokrasia ya mwananchi pia kuanzisha, kujenga na kuendeleza taasisi mpya endapo haridhiki au hakubaliani na zile zilizopo.

Hili linadhihirisha kwa wabunge na mawaziri wetu kwamba yale yanayofanyika leo katika kuinyima sehemu fulani ya jamii haki zao kwa upande mmoja lakini wakati huo huo kwa upande mwingine wabunge na mawaziri hao kuipa sehemu nyingine sio tu haki zao tu bali na ziada isiyodaiwa pia.

Huku hakuwezi kutafsiriwa kwa namna nyingine ila ni dhuluma na uonevu kwa yale makundi yanayonyimwa haki na maslahi yao mchana kweupe.

Aidha kitendo cha kuwa na bodi au mamlaka kuwalangua wakulima na kuwakatisha tamaa katika shughuli zao za kilimo hakutafsiriki kwa njia nyingine yoyote ile ila ni wizi wa jasho la mkulina na dhuluma na uonevu kwa waliomo katika sekta ya ukulima, uvuvi na ufugaji. Haki hapa ni kwa watu hawa kuwezeshwa kama wenye viwanda walivyowezeshwa kuzalisha na kuuza wao wenyewe kile wanachokizalsha.

Wafanyakazi wanapoamua hili au lile ili kupigania haki na maslahi yao na kisha kuingiliwa na mahakama au polisi pia hakuwezi kutafisrika kwa njia nyingine yoyote ile ila ni dhuluma na uonevu kwa wafanyakazi wa nchi hii. Mfanyakazi mmoja mmoja na kwa pamoja wana haki saa yoyote, wakati wowote na mahala popote kuonesha kutoridhika na hali ilivyo au uamuzi fulani na ni ruksa kwao kukutana, kuandamana, kupinga na kuonesha kilio na kutoridhika kwao.

Wachimbaji madini wana haki ya kidemokrasia ya kutafuta riziki yao ya kila siku. Na pale mgodi unapopewa ardhi ambayo wachimbaji wadogo ndipo walipokuwa wakipatia riziki yao wachimbaji hao wadogo wana kila haki ya kulipwa fidia ya kutosheleza riziki yao ya kila siku kwa miaka yao ya uhai iliyobakia.
Kinachofanyika sasa sio tu ni mauaji yanayobarikiwa na wakubwa, dhuluma na uonevu bali unyang'anyi wa mali ya Mtanzania unaofanywa na wageni toka nje.

Kuna wanojiuliza hivi haki ya wanawake kuwa na makundi yao ni kwa CCM tu. Huu sio ubaguzi wa kijinsia kwa wanawake wasiokuwa wanachama wa chama fulani na kilichoshika pochi la taifa ? Kwanini tulilikataa Baraza la Wanawake wa Tanzania lilikosudiwa kuwa mwamvuli wa makundi ya aina yote ya wanawake katika jamii yetu. Hivi tunaamini kuna kundi la wanawake katika nchi hii wanaostahili kuneemeka wao peke yao na neema mbalimbali zinazokuja Tanzania toka ndani na nje ya nchi ?.

Vijana kuanzia Arusha hadi Zanzibar wameachwa kwenye mataa na watawala waliopo. Maana vijana wenye maana ni wale wa chama tawala tu. Kutokana na hili wale wasiokipenda chama hicho wana wakati mgumu katika kujikwamua kiuchumi na kijamii. Je, hili ni sawa. Na kweli katiba inayovumilia jambo hili ni katiba yenye haki, usawa na uhuru kwa watu wote ?

Utengwaji huu wa vijana kutokana na ubaguzi wa kisiasa au kichama umechangia sio haba kwa Zanzibar kuwa na 'teja' kwa karibu kila familia visiwani humo.

Kutokana na kundi la Wazee lililokuwepo kuwa na mwegemeo wa kisiasa kuna wazee kadhaa waliodhulumiwa na wanaoishi maisha ya dhiki na ya umasikini mkubwa leo lakini kundi hilo la wazee la kichama sio tu haliwajulii hali bali pia halina mpango wa kuwasikiliza achilia mbali kuwasaidia katika kupigania haki zao. Tunalojifunza hapa ni umuhimu wa wazee wa kila eneo kuwa na chombo chao kwa ajili ya kupigania haki na maslahi zao wakingali hai na sio pale wanapokwishakufa. Wazee wa kisiasa wakati wa sakata la wastaafu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki walikaa kimya kama hilo jambo haliwahusu kabisa. Lakini ni vyema hapa wazee tukakumbushana kwamba ukimuona mwenzio ananyolewa na wewe tia kcihwa chako maji.

Wanafunzi nao wanasukwasukwa na kulazimishwa kuwa katika makundi maalum ambayo yanaishia kwa viongozi wake kushirikiana na wale wanaowakandamiza na hivyo kufanya shule na vyuo vyetu sikuzote viwanja vya migogoro na mapambano badala ya mahala vijana hao wanapoweza wakati mwingi kusaidia kufanya tafiti mbalimbali za kuiendeleza nchi hii na watu wake.

Faida za vikundi huru vya kijamii na kiimani

Kuna faida mbalimbali za kuwa na vikundi huru vya kijamii na kiuchumi katika nchi:

Kwanza, vinapanua wigo wa kutatua matatizo ya kijamii na kutumia fursa za kiuchumi na kijamii zilizopo kwa makundi mbalimbali ya watu katika jamii,

Vikundi huru vya jamii na hasa pale vinavyopewa nafasi ya uwakilishi vijijini,mjini, tarafani, wilayani , mikoani na kitaifa vinawezesha sauti ya kila mtu kusikika,

Ni njia ya uhakika na ya kuaminika zaidi ya kupanua, kuendeleza, kujenga na kuimarisha demokrasia katika ngazi ya chini ya taifa hadi ile ya juu kabisa,


Makundi huru ya jamii yanasaidia kuondoa kutawaliwa makundi na chama chochote cha siasa,

Vikundi huru vya jamii pia vinasaidia kuondoa kutumiwa kwa vikundi na wanasiasa kama ilivyofanyika kule Kenya, Zimbabwe na nchi nyingine za Kiafrika zinazobeza, kudumaza na kulemaza demokrasia,

Vikundi kama hivi vinasaidia pia kupunguza rushwa na hongo za kisiasa kwa kuwa vinajenga uwezo wa watu kujikidhi wao wenyewe mahitaji yao yote ya msingi na kinachobakia kwao sio njaa na ukata bali ni kutafuta kuendelea juu zaidi,

Vikudni vya kijamii vikijiingiza katika miradi ya ujasiriamali jamii vina uwezo mkubwa pia wa kutoa ajira kabakaba kwa vijana, wanawake na hata wazee wasiokuwa na kazi,

Vikudni vya jamii vina uwezo mkubwa wa kuchangia katika kuendeleza rasilimal watu bila hili kuwa na ila au njama ya aina yoyote ile kwa vikundi vingine katika jamii tofauti ilivyo na pale dini fulani inapotaka kupora kazi hii toka serikalini na kuifanya wao,

Vikudni vya kijamii vinavyofanya kazi na vinavyojua wajibu wao na Utaifa na Uzalendo wao vina kila sababu ya kuzuia wanasiasa na wafadhili toka nje kuwatumia viongozi wa makundi fulani,

Aidha ni vikundi hivi aghalabu vinavyovuka upofu na uoni mfupi wa viongozi wasiojua taradadi na tarajali za jamii ndivyo vinavyoweza kuzuia Taasisi za kidini kutumia ombwe linaloachwa na Serikali dhaifu ili kudhulumu dini nyingine katika masuala ya elimu, afya na huduma za jamii.

Fedha ya mlipa kodi itumike kupeleka demokrasia vijijini na sio kuiua demokrasia vijijini.

Sunday, July 12, 2009

DEMOKRASIA NA UHURU WA KIUCHUMI NA KIJAMII KWA MAENEO NA WATU

AFRIKA ya leo sio ya jana. Huko nyuma wananchi katika nchi nyingi za Kiafrika waliwachukulia viongozi wao kama vile viongozi hao walikuwa BABA zao. Na viongozi hao waliona raha kuitwa baba wa taifa au baba wa hili au lile. Ingawa kwa kiasi kikubwa ni wachache sana kati yao walioweza kutimiza wajibu wao kama baba. Baba alitarajiwa kuwafanyia wananchi (wanawe hata kama wa kufikia) yale yaliyo ya baraka, heri na wema wa dhati toka ndani ya moyo wa mtu. Baba alitakiwa kuwa kielelezo cha utu na ubinadamu. Haikutarajiwa hata siku moja kuwa baba atakuja geuka kuwa mtu anayependelea kati ya wanawe; atawaibia wanawe; atawadhulumu wanawe; atawasingizia uongo wa kutupwa wanawe; atawanyanyasa na kuwatesa wanawe; hatafanza ubaguzi kati ya wanawe; atawagandamiza wanawe; atawadhulumu wanawe; atawaonea na hata kuwaua wanawe.

Kwa bahati mbaya BABA wa jana na wa leo Afrika anayafanya madhambi haya hapo juu kila siku. Na mwananchi amechanganyikiwa na anajiuliza amwamini na amtegemee nani sasa.

Tatizo kubwa la Ubaba ni lile la kutaka kusimamia NYUMBA KUBWA YENYE VYUMBA ZAIDI YA 50 AU SHAMBA LA HEKTA ELFU lakini wewe unajua na unatumia tu vyumba viwili au vitatu katika jumba hilo au moja ya nane ya hekta katika shamba hilo.

Kinachotokea kwingine huna habari nayo. Labda uletewe na mtu habari. Na mjumbe huyo mara nyingi huleta uongo au habari za kupkwa. Na wewe kwa kuwa huna muda aghalabu utakuwa unaukubali uongo kuwa ukweli. Matokeo yake mpaka funza anatoka kwenye dole huku kaacha watoto milioni mwilini mwako ndio unagutuka, ala, kumbe kidoleni kuna mama wa mafunza!

Uhuru wa Mikoa na Demokrasia

Wapigania demokrasia hawataki uhuru wa mikoa eti kwa sababu wanataka kuigawa nchi au kuvunja umoja na mshikamano katika nchi. Mungu aepushilie mbali hayo. Wanataka uhuru kwa mikoa ili tujenge umoja na mshikamano imara zaidi kutokana na kutumika kikamilifu fursa za kiuchumi na kijamii zilizoko katika kila mkoa. Mikoa kama inakosa ubunifu na ujasiriamali na utundu wa kujaribu mambo mapya na ikazalisha kidogo basi keki ya taifa inakuwa ndogo. Mikoa ikijititimua na kuzalisha zaidi na keki ya taifa nayo inakuwa kubwa kila siku.

Na uhuru wa kiuchumi na kijamii hauwezi kupatikana kupitia meza ya katibu mkuu wa wizara ya serikali za mitaa au wizara kama hiyo. Uhuru wa mkoa unapatikana kwa njia moja tu. Kila mkoa kuendesha uchaguzi wa kumchagua Gavana wake au Kiongozi wao wa mkoa, wawakilishi wao na wajumbe wao wa ngazi za chini. Gavana atachagua mionngoni mwa wabunge wa mkoa husika mawaziri wa serikali itakayosimamia masuala ya uchumi na jamii ya mkoa husika. Kwa kitendo cha siku moja safari ndefu ya kuwa na mikoa inayojiendesha kiuchumi na kijamii itakuwa imeanza. Kwa saini moja tu ya Mkuu wa nchi demokrasia itakuwa imesimika mizizi ya kweli kuanzia vijijini na miji katika kila mkoa. Kwa sheria moja tu toka bunge la taifa kila mkoa utakuwa na wawakilishi wake wanaojua ni wapi kiatu kinafinya na wanaozungumzia kila kwenye kikao matatizo na ufumbuzi wa matatizo ya wananchi wanaowawakilisha na sio porojo, umbeya, uzushi na ngonjera zisizo kwisha.

Ipo hatari pia ya kujilimbikizia mamlaka iwe yale ya kisiasa, kiuchumi, kirasilimali au kifedha.
Badala ya kutumika vyema aghalabu hutapanywa. Na hiki ndicho kinachotokea kutokana na sakata ya B.O.T., EPA, baadhi ya dini kugawana fedha za wafadhili na serikali na kashfa nyingine katika wizara, taasisi na mashirika mbalimbali ya kiuchumi na kijamii nchini.

Kwa kuwa nchi ni kubwa na watu ni wengi vibilioni mia au mia mbili au mia tatu ikivigawa vinakuwa havina uwezo wa kubadili maisha ya yeyote ila kwa yule mchotaji anayewahi kutoka na tonge kubwa kabla hicho kilichotolewa hakijaanza hata kugawiwa.

Kinachotakikana hapa sio fedha bali uhuru wa kiuchumi na kijamii kwa wananchi huko huko mikoani na majimboni walipo kukaa chini na kuweka mipango na mikakati yao ya maendeleo na kukusanya nguvu zao za mwili na za kifedha kuleta mabadiliko yanayoweza kukifanya kidogo kuwa sio tu kikubwa bali kinachojizalisha na kujiendeleza chenyewe na hivyo kuwahakikishia wakazi wa mtaa, kata, tarafa, wilaya au mkoa maendeleo endelevu. Kinyume cha hivyo kama nchi ilivyo tegemezi kwa wafadhili basi mikoa nayo itaendelea kuwa tegemezi kwa serikali na kuwa vipofu kwa fursa pekee za kiuchumi wanazoweza kuzitumia wao wenyewe na kuondokana na utegemezi huu unaotulemaza na kutudamaza takriban karibu miaka hamsini kufikia sasa.

Demokrasia ya kweli
Demokrasia ya kweli itatokana tu na kila Mkoa kuwa na Gavana au kiongozi wake wa kumchagua na sio wa kupachikwa na chama chochote cha kisiasa kiwacho au serikali iliyoko madarakani. Kazi za serikali ni kusimamia wizara kisiasa na kiutawala na sio kusimamia mikoa kiuchumi na kijamii.
Kazi ya kusimamia maendeleo ya kiuchumi na kijamii ya mkoa inastahili kufanywa na Gavana wa mkoa, mawaziri wa mkoa na wabunge wa mkoa. Hawa wamevaa kiatu husika na wanajua kinachofinya. Vinginevyo kazi hii ikifanywa katika ngazi za wizara, basi tutaishia kila waziri kutaka kupeleka miradi yote ya wizara yake katika mkoa wake kama sio jimbo lake la uchaguzi.

Gavana wa mkoa hatakuwa muuza siasa na sera bali mtendaji mkuu wa kiuchumi na kijamii. Mkoa utakuwa ni kampuni na yeye ni Mkurugenzi au Meneja Mkuu. Wakazi wa mkoa watategemea awe na mawaziri wa vitendo na sio wa maneno. Kama kuna waziri wa maji na umwagiliaji basi waziri huyo atahakikisha kila sehemu mkoani wanapata maji na kuna umwagiliaji maji. Kama ni waziri wa Viwanda na Biashara basi waziri huyo wa mkoa atahakikisha mkoa unapata wawekezaji ndani na nje ya nchi ili mkoa uwe na viwanda inavyovihitaji na vinavyoingiza faida na sio hasara au kugeuzwa kuwa maghofu au karakana au ghala za wafanyabiashara, wenye viwanda, taasisi zisizo za kiserikali na kadhalika.

Wabunge wa mkoa watakuwa ni wawakilishi wa maeneo ya watu kati ya 50,000 na laki mbili nao kazi yao kubwa itakuwa ni kuhakikisha sauti ya wananchi wake ndiyo inayotawala katika maamuzi na utekelezaji wowote wa masuala yanayohusu eneo lake. Jimbo lake litashindana na majimbo mengine mkoani kwa kuhakikisha wana rasilimali watu tosha, barabara nzuri, maji, umeme, mazingira bora kwa wawekezaji wa ndani na nje na vitu kama hivyo.

Kwa kufanya hivi kila jimbo, kila wilaya na kila mkoa utakuwa unapambana kuwaondoa watu wake toka kwenye umaskini unaowanyima haki yao ya kuchangia katika demokrasia na maendeleo ya kweli ya nchi na watu wake.

Katika hali tuliyonayo ambayo makosa ya serikali na yale ya wanasiasa yanaendelea kumasikinisha baadhi ya mikoa haitakuwa rahisi kujenga na kuimarisha demokrasia katika maeneo mengi katika nchi zetu za Kiafrika.

Bila umasikini wa kutupwa kuondoka itakuwa ni ndoto kutarajia kujengwa kwa demokrasia ya kweli na inayofanya kazi.

Hii ni demokrasia itakayoruhusu pamoja na mambo mengine mkulima kuuza mazao yake ndani na nje ya nchi; mvuvi kuuza samaki zake ndani na nje ya nchi; mwenye mali asili kama miti au madini kuuza alichokitafuta kwa gharama na kukipata ndani na nje ya nchi; Watanzania kuwa huru kufanya kazi au kwenda kucheza michezo nje ya nchi bila kuwekewa mikwara na mtu au taasisi yoyote.

Ni demokrasia ya kijamii na kiuchumi itakayowadhihirishia Watanzania kuwa anga ndio paa la matamanio na makusudio yao na yeyote anayewakwaza ni adui wa na adui wa taifa.

© 2009 Sammy W.I.Makilla

Saturday, July 11, 2009

DEMOKRASIA NA UWEZESHWAJI WA VYAMA VYA UPINZANI

HAIWEZEKANI kuwa na demokrasia ya kweli katika nchi nyingi za Kiafrika kutokana na nguvu kubwa iliyo nayo chama tawala ukilinganisha na udhaifu mkubwa wa vyama mbadala.

Kubwa zaidi ni kukosa uwezo wa kuwa na ofisi katika kila wilaya, mji na kijiji; pia kukosa uwezo wa kuwa na vyombo vya usafiri vinavyofaa na kutosheleza mahitaji yao; hali kadhalika, kuwa na fedha za kutosha kuwalipa baadhi ya watendaji wao ili washughulike na kazi moja tu ya kukijenga chama na uwezo wake wa kuchangia maendeleo ya nchi na watu wake.

Kwa sababu hii ninashauri watu wote ikiwemo wafadhili toka nchi za nje kwamba wakati umefika sasa wa kusaidia vyama mbadala kuwa na msingi bora na imara wa kuanza kushirikisha kikamilifu na kwa dhati katika siasa za vyama vingi nchini.

Ninapendekeza msaada huu usiwe ni sadaka bali ni mkopo wa riba nafuu na utakaolipwa baada ya miaka 20 au zaidi. Mikopo hiyo iwawezeshe wanasiasa na vyama vya siasa mbadala kujenga ofisi ambazo pia zitakuwa na vyumba au ghorofa za kukodishwa ili kuviingizia pato kila mwaka; vyombo vya usafiri na fedha za mbegu za kusimika vyema mizizi ya vyama hivyo hasa huko wilayani na vijijini.

Uhalali wa vyama mbadala kusaidiwa katika hili unatokana na ukweli huu hapa chini:

Vyama tawala vingi vilikuwa na miaka 35 au zaidi ya kujilimbikizia ukwasi na mali za kila aina wakati vyama mbadala havina zaidi ya miaka 10 toka vianze kutafuta wapi pa kuanzia. Isitoshe vyama tawala vinavibana vyama mbadala kwa kila hali ili visijenge na visiwe na uwezo kama wao wakijua fika kwamba kwa kuwaachia wapinzani kuwa na nguvu basi utakuwa ni msiba kwao. Kwa hiyo hatuwezi kutarajia serikali ya chama tawala fulani kusaidia kuimarisha chama cha upinzani waziwazi. Ingawa hili halizuii mtu mmoja mmoja katika chama tawala kusaidia chama hiki au kile mbadala kwa sababu moja au nyingine.

Aidha vyama vingi tawala kwa kupitia kisingizio cha ujamaa na utafa vilipora mali za wananchi na kuzifanya mali za chama. Hadi wa leo hakuna chama chochote tawala kilichokiri hili na kuzirudisha mali hizo ila pale ambapo chama hicho kimeondolewa madarakani na mahakama au wananchi wenyewe kudai na kunyakua kilichokuwa chao.

Vyama vingi tawala Afrika vimejenga nyufa na mianya makusudi ili kuiba fedha toka Hazina, bima, pensheni, mfuko wa usalama wa jamii, wizarani, serikali za mitaa na mashirika kama hayo kwa namna ambayo chama hakihusishwi kabisa na wizi huo ingawa kwa yakini mwizi ni chama na sio hao wanaotumiwa na wanasiasa na makuwadi wao wa fedha haramu wanazoibiwa wananchi wakiwemo wanyonge kama wazee, mayatima, wagonjwa, wanavijiji, walemavu na wengine kama hao.

Kwa kutumia mamlaka za kodi aidha vyama tawala katika nchi nyingi huwafanya wafanyabiashara na wenyeviwanda na wawekezaji ama kwa kupenda au kushawishiwa kiujanja au kulazimishwa au kwa kutoa rushwa kuvipatia fedha vyama hivyo kwa mihadi kwamba mali zao zitaongezeka pale chama kinaporudi madarakani.

Fedha nyingi ambazo vyama tawala vinapata hazitumiwi ili kuwaelewesha wananchi vijijini kwamba vyama vingi na demokrasia ni jambo zuri kwa nchi zetu bali hutumika kwa kazi kinyume cha hiyo. Aghalabu fedha hizo hutumika kuwaghilibu wananchi kwamba watakuwa maskini zaidi, wataingia katika matatizo makubwa na pengine hata watauawa wakichagua chama kingine kutawala nchi.

Ni vyama mbadala vichache sana ambavyo watumishi wake wana mishahara au uhakika wa kipato jambo ambalo ni tofauti kwa upande wa vyama tawala. Uhakika huu kwa vyama tawala unawapa watumishi wake jeuri, kiburi, tamaa na ulafi wa kupata zaidi na dharau ya kuwaburuza wananchi. Wakati unyonge huu unawapa watumishi wa vyama mbadala matende ya kuthubutu na kujaribu yale yanayoweza kuendeleza na kuimarisha upinzani nchini.

Hoja hizo hapo juu ni tosha kuonesha kwanini wazo la kuvisaidia vyama mbadala viwe na miguu yake vyenyewe ni suala muhimu na yakini ndio stata ya upinzani wa kweli katika nchi nyingi za Kiafrika.

Ili kukuza na kuimarisha demokrasia Afrika ni muhimu mambo haya yafanyike:
. Vyama mbadala viwezeshwa kuwa na majengo ya ofisi tarafani,wilayani, vijijini, kata, mitaani ili sio tu kuwa na makazi maalum yanayotambulika na kuheshimika lakini pia vyanzo vya mapato ya kila mwaka ya uhakika ili kuondokana na tamaa ya rushwa au misaada inayoua demokrasia badala ya kuijenga.
. Ni muhimu pia kwa kutambua ukubwa na upana wa nchi hii kwa vyama mbadala kupewa misaada na mikopo itakayowawezesha angalau kuwa na vyombo vya usafiri ambavyo vinaweza pia kukodishwa na kuingizia mapato chama wakati visipohitajika kwa shughuli za kichama.

. Ni muhimu watu kama Westminster Foundation for Democracy, George Soros Foundation, USIS na Umoja wa Mataifa kuangalia uwezekano wa kutoa mikopo au ruzuku katika miaka ya mwanzo ili angalau sehemu nyeti ya wafanyakazi wa vyama mbadala vya kisiasa kuwa wanalipwa mishahara.

. Hili liende sambamba na wahisani kusaidia kujenga uwezo wa menejimenti na utawala ili waweze kusimamia mambo yao kisayansi na sio kisanii.

. Hili linaweza kufanyika vizuri zaidi kama kila chama kitakuwa na mpango wa kuandaa 'Strategic Planning' yake kwa shughuli za ndani za kichama na ile ya kukikuza na kukiimarisha chama kitaifa.


Pamoja na mambo mengine Mpango huo wa Kimkakati utavisadia vyama hivyo kuwa na miundo na mifumo ya vyama isiyo na matatizo na inayokwenda na wakati.

Yumkini wanasiasa wengi wa vyama mbadala wanaonekama kama watu waliochanganyikiwa, wenye matatizo yasiyokwisha, masikini na watu wenye njaa kali sio kwa sababu vyama mbadala vinataka hivyo ila kwa sababu chama tawala na serikali vinafanya makusudi ili waonekane hivyo. Hii ni tofauti kabisa na huko Ulaya na nchi nyingine zilizoendelea kidemokrasia ambako viongozi wa vyama mbadala hawachukuliwi tofauti na wale wa vyama tawala kwa kiasi hicho.

Ni dhahiri basi kwamba endapo vyama mbadala vitapata mikopo au misaada ya kufanikisha mambo hayo hapo juu hawatashindwa kuwajulisha wananchi kwamba vyama vingi ni kitu kizuri kwao na sio jambo baya kama vile vyama tawala Afrika vinavyofanya lionekane kwa hivi sasa.

Mapendekezo yangu ni kwamba pawe na:
MFUKO WA KUWAJENGEA VYAMA MBADALA AU UPINZANI MISINGI IMARA YA USHINDANI WA KISIASA KATIKA NCHI ZA KIAFRIKA KAMA INAVYOFANYIKA HUKO ULAYA KWA MSAADA WA BW. GEORGE SOROS.

Mfuko huo utoe mikopo ya riba nafuu ili angalau vyama mbadala vijenge ofisi moja kubwa katika ngazi ya mkoa na moja kila wilaya na kisha ndogo ndogo kwa kila tarafa.

Ofisi zote zipatiwe vifaa na zana muhimu za kazi.

Wakopeshwe fedha za uendeshaji kwa miaka 3 na kisha baada ya hapo baada ya kufundisha jinsi ya kukodisha baadhi ya vyumba katika majengo yao mbinu za ujasiriamali jamii ili waweze kuendelea na kazi ya kujenga na kupanua vyama vyao wao wenyewe.

© 2009 Sammy W.I.Makilla