INDIA, taifa lenye kufuata demokrasia na lenye watu wengi kuliko mataifa mengine duniani yanayofuata demokrasia mwaka huu kwa mara ya kwanza liliweza kuendesha uchaguzi wake mkuu kwa kutumia TEKNOHAMA.
Nchi hiyo imedhihrisha inawezekana kabisa kuondoa mkono wa mtu unaolaumiwa sana kwa kupandikiza majina ya uongo katika daftari la wapiga kura, kutowaandikisha wapiga kura walio na haki ya kupiga kura, kuingiza kura za uongo, kuharibu na kupoteza kura za halali na mambo mengine kama hayo.
Jambo hili linaashiria kwamba ikiwa patakuwa na muundo na mfumo unaokubalika wa Katiba mpya katika mfumo wa vyama vingi na Tume Huru isiyoegemea upande mmoja na kisha kutumiwa TEKNOHAMA haki na usawa katika upigaji kura ni mambo yanayoweza kuwa kitu cha uhakika zaidi kuliko ilivyo sasa.
Katika nchi nyingi za Kiafrika kile kinachoitwa Tume ya Uchaguzi ni kiumbe cha chama tawala na seriklai yake. Ni zao la Katiba za viraka na ziizopitwa na wakati. Ni zao za sheria zilizopitwa na wakati na zisizokidhi matarajio ya ushindani wa kisiasa, soko huru na haki za binadamu.
Kwa kuwa wanaoongoza taasisi hizo ni watu wanaolishwa fadhila na chama tawala matokeo yake sikuzote ni kukisaidia na kukipendelea chama hicho kishinde hata pale kinapostahili kushindwa.
Uhakika wa kura ya mpiga kura kwenda kwa yule anayemtaka, Haki na Ukweli ni vitu vinavyowezekana endapo kutakuwa na upigaji kura kieletroniki.
Madhali nchi kama India imeshaanza kazi kama hii kinachotakiwa ni kwa chombo cha Umoja wa Mataifa kinachoshughulika na Demokrasia na Haki za Binadamu kuwa wakala wa kukodisha vifaa vya Teknohama toka India ili vitumike wakati wa uchaguzi katika nchi mbalimbali za Kiafrika na dunia ya tatu kwa ujumla.
Vinginevyo, utafiti uendelee kufanyika zaidi ili kuja na mashine bora zaidi za kieletroniki zitakazoondoa kabisa wizi na ujanja wa aina nyingine wakati wa kupiga kura Afrika na duniani kote kwa ujumla.
Ikumbukwe kwamba WIZI NA RUSHWA KUBWA KULIKO ZOTE ni zile zinatokea wakati wa chaguzi katika nchi mbalimbali Afrika. Ukkomesha wizi na rushwa hii katika ngazi hiyo utakuwa umelisaidia bara hili sio haba.
Nini kifanyike
Serikali ya India ambayo kwa sasa iko karibu na nchi za Kiafrika kuliko wakati wowote uko nyuma inaweza kuanza kwa kuwaalika wanasiasa na vijana wa vyama mbalimbali vya kisiasa kwenda India ili kupata mafunzo ya muda mfupi kuhusu upigaji kura kielektroniki. Huko watajifunza kwa nadharia na vitendo na hivyo kutambua uboa na udhaifu wa njia hiyo ya kupiga kura. Endapo wataona ni jambo linaloifaa Tanzania basi bila shaka watakuwa na hamasa ya kuja kulieleza, kulieneza na kulifanya likubalike hapa Afrika kwa urahisi.
Kama shabiki wa Teknohama nimekuwa nikijiuliza hivi kuna uwezekano wa kuwa na sanduku la kura lenye kutumia betri na linaloweza sio tu kupokea kura bali kuhakikisha halikubali kura mbaya na kisha kupiga hesabu ndani kwa ndani na kuonesha kwenye skrini juu yake kila mgombea kapata kura ngapi? Kisha boksi hilo liwe na uwezo wa kutuma majibu hayo kioto kwenda kwenye kompyuta kuu ya uchaguzi kiwilaya, kimkoa na kitaifa ?
Boksi hilo litakuwa na uwezo pia wa kuainisha vidole vya mpiga kura na kama namba yake inaendana na alama hiyo anakubalika na kama sivyo anakataliwa?
Simu za Mkononi
Kuna wanaofikiria pia upo uwezekano wa kutumia simu za mkononi maalum au za kawaida katika uchaguzi mkuu na upigaji kura wakati wowote.
Simu maalum za kupiga kura zitakuwa ni simu ambazo zinatumika kwa ajili hiyo tu na taifa litawajibika kumnunulia kila mpigaji kura simu yake kutokana na kodi za wananchi. Simu hiyo itanunuliwa mara moja tu katika maisha ya mtu. Na wale wanaokufa zitarekebishwa ili wapewe wapigaji kura wapya wanaoingia kwenye orodha ya wapiga kura baada ya kutimiza umri wao.
Aidha kwa simu za kawaida baada ya wananchi kuandikisha simu zao zote itachaguliwa namba moja mama itakayokubalika katika kupiga kura na masuala mengine ya kijamii na kiuchumi katika mfumo maalum wa kurahisisha na kupanua matumizi ya simu za mkononi.
Kwa kutumia namba ya simu yako iliyoandikishwa na inayokubalika baada ya kila kitu kuthibitishwa utaweza kupiga kura yako ukiwa unastarehe nyumbani kwako bila ya kwenda mahala ukacheleweshwa, kunyeshewa na mvua na kuchomwa na jua bila ya sababu ya maana. Jambo hili sio tu litawapa nafuu kubwa wapiga kura lakini pia litachangia idadi kubwa ya watu kupiga kura wakati wowote upigaji kura unapohitajika bila ya kugonja miaka mitano.
Itakuwa ni rahisi pia kufanya chaguzi ndogo kwa sababu gharama yake itakuwa ni ile tu ya uratibu na mawasiliano.
Kwa kifupi, Waafrika ambao ndio wanaokabiliwa na tatizo hili la wizi wa kura wanastahili kuwa mstari wa mbele kutafuta ufumbuzi wake. Mawazo haya ninaamini yanaweza yasifae au kukubalika lakini lengo langu la kuamsha mjadala kama Teknohama inaweza kutusaidia kuwa na chaguzi za huru, haki na zenye ukweli zaidi litakuwa limefanikiwa.
Sunday, July 26, 2009
Subscribe to:
Post Comments (Atom)

No comments:
Post a Comment