KUNA wanaodai kuwa hakuna nchi inayopenda wananchi wake wazinduke na kufahamau kuwa demokrasia Afrika sio kitu kibaya bali ni jambo zuri na litakalowasaidia watu kubadili maisha yao.
Kwa sababu hii Afrika nzima inalalumiwa kwa kuwafanya watu wa vijijini waendelee kuwa wajinga kuhusu haki na uhuru wao wa kidemokrasia.
Haiwezekani kabisa kuwa na demokrasia ya kweli hadi wananchi vijijini waelewe kuwa chama tawala sio baba wala mama au taasisi ambayo ikiondoka basi na wao ndio utakuwa mwisho wao.
La. Chama Tawala kilichopo na vingine vitakavyokuja ni taasisi zitakazostahili kuwepo tu kama zitawafanyia wananchi kazi nzuri inayoonekana na wote. Kama sivyo, ni ruksa kukikataa chama chochote ili chama mbadala kishike nchi ili nacho kijaribu kutumikia watu kwa utii na uaminifu zaidi. Nacho kikiboronga pia fimbo ya kura itakichapa na vitaendelea kujirudi na kujirekebisha vivyo hivyo mpaka angalau kimojawapo kiweze kufanya kazi iliyotumwa na wananchi.
Ni muhimu kwa serikali zetu kuondoa kodi na mikwara yote inayosababisha magazeti, redio, televisheni, vitabu na machapisho mengineyo kuwa ghali kuliko uwezo wa wananchi wengi vijijini.
Na wafadhili na wanaoitakia nchi hii mema ni lazima wasaidie uanzishwaji wa magazeti, redio na televisheni za jamii ambavyo kazi yake kubwa itakuwa ni kuwaamsha watu vijijini juu ya ukweli kuhusu haki, uhuru na demokrasia katika nchi yao.
Aidha ni haki ya wananchi kudai kuwa fedha zinatokana na kuchimbwa kwa dhahabu, almasi, tanzanite na madini mengineyo kiasi fulani kitumike katika kuhakikisha kuwa elimu ya msingi, sekondari na chuo kikuu kwa kiasi fulani inakuwa bure.
Watoto wetu kuwa na elimu ya angalau sekondari [inayotolewa bure au kwa gharama nafuu sana] ndio mwanzo sio tu wa kujenga taifa lenye kujali na kufuata demokrasia bali pia msingi imara wa watu wenye ufundi na ujuzi unaohitajika na wawekezaji wa ndani na nje.
Juu ya yote, binafsi, ninaamini kuwa lazima elimu ya chekechea hadi Chuo Kikuu hapa Tanzania iwe inatolewa kwa lugha ya Kiswahili na Kiingereza.
Anayetaka kusoma kwa Kiingereza awe na haki hiyo. Na anayetaka kusoma kwa Kiswahili naye asinyimwe haki hiyo.
Ni dhahiri mataifa koloni kama Uingereza na Marekani yatapenda sana Tanzania idharau Kiswahili kwani kwa kufanya hivyo tutabakia kuwa koloni lao daima dawamu.
Tukiiga mfano wa China, India, Malaysia, Korea, Japani na wengine kama hao ni hatari kwao maana tutajiondoa kwenye makucha yao haraka kuliko wanavyotaka.
***
Sunday, June 15, 2008
Subscribe to:
Post Comments (Atom)

No comments:
Post a Comment