AFRIKA imekuwa kwa miaka mingi ikitumia vyombo vya habari vinavyomilikiwa na serikali kama vyombo vya kuwaacha watu wao katika giza kuhusu masuala mbalimbali ya kitaifa.
Demokrasia ya kweli haiwezi kupatikana kama mhimili huu muhimu wa nne hautaheshimiwa na kuacha kufanya kazi zake bila kuingiliwa na mtu yeyote isipokuwa kwa zile sheria na kanuni ambazo vyombo vya habari vimejiwekea kitaifa na kimataifa.
Vyombo vya habari ni walinzi wa demokrasia. Na vikiachiwa kufanya kazi zao bila kuingiliwa au kushawishiwa na walioko au wasioko madarakani vinaweza vikatoa mchango muhimu katika kuwapatia wananchi habari zilizo wekwa katika mizani vyema na kuwaachia wananchi wenyewe wafanye maamuzi kutokana na habari walizo nazo.
Ni ufujaji fedha bure kama vyombo vy a habari viwe vya serikali au chama au watu binafsi vitakuwa vinatumiwa na walioko madarakani ili kufunika ukweli na kupaka nyumba mbovu rangi staii ya wenye simu za mkononi. Kibovu ni kibovu tu, kibaya ni kibaya tu, ukweli ni ukweli tu! Na yule anayeamini kuwa kaitwa mbovu naye ni ngangari; au kaitwa mbaya naye ni mzuri basi akavishtaki vyombo vya habari kwenye mhimili wa tatu, yaani, mahakama.
Juhudi zinazofanywa na serikai nyingi Afrika katika kuvidhibiti vyombo vya habari zinadhihirisha uozo na ubovu wa serikali zinazofanya hivyo katika vita vya kuwaondoa watu wao kutoka kwenye umasikini, ujinga na maradhi.
Ukiachia serikali yoyote kuvidhibiti vyombo vya habari, kuwanyanyasa waandishi wa habari ni kuachia serikali na chama tawala hatimaye kudhibiti watu wote na kuwanyanyasa watu wote na mwisho wa yote kuliingiza taifa husika katika vita vya wenyewe kwa wenyewe na machungu yanayoandamana na hilo.
Hapana sababu yoyote ya Afrika kushindwa kuheshimu na kufanya kazi kwa uelewano mkubwa na vyombo vya habari kwa faida ya wananchi wote.
Mara kadhaa ukiona waandishi na vyombo vya habari vinaandamwa hapa Afrika lazima kuna baya lililonaswa ma walioko madarakani wanatumia fedha za umma kujikosha mbele ya dunia.
Mathalani, mwaka 1994 kuelekea Uchaguzi Mkuu wa kwanza wa vyama vingi Watanzania toka kampuni ya Business Times Limited walifikishwa mahakamani kwa kosa la uhaini. Kosa lao eti lilikuwa ni kuanika uwazi kuhusu rada mbovu serikali na chama tawala wakati huo vilivyopanga kuinunua. Miaka michache baadaye imegundulika kuwa rada hiyo sio tu ilikuwa mbovu bali pia kuna rushwa iliiyotembezwa na Waingereza hapo pia.
Katika hali kama hii kuwa kwa upande mmoja kuna serikai inayoweza kutumia nguvu za dola kumsingizia mtu uongo na upande wa pili kuna watu walioko tayari kujitoa mhanga ili ukweli ujulikane haiwezekani kwa serikali hiyo hiyo kuwachukulia hatua waandishi au wachapishaji. Lazima apatikane mtu wa tatu kuja kuamua ugomvi huu, maana ugomvi hii ni wa watu wawili--mmoja serikali na mwingine vyombo vya habari ambao wote wana haki sawa katika kutetea haki za umma. Haiwezekani serikali wakati wowote ikaonekana kuwa ni takatifu na wengine ni wachafu labda kama kuna hila fulani inayofichwa na viongozi husika.
Nchi inayotaka kufuata demokrasia ya kweli na ya uhakika; uwazi katika uendeshaji wake; isiyo na jambo la kuficha na inayopigania haki za wengi na sio kundi la wajanja wachache haiwezi kamwe k uhitaji Wizara ya Habari! Maana kazi hii tayari ina wenyewe na tena wanaifanya uzuri sana. Kinachohiajika ni sekta hiyo kuwa kamilifu kwa kuwa na vyombo vyote vya kusimamia na kuendesha mambo yake kwa ufanisi na ufanifu zaidi.
***
Sunday, June 15, 2008
Subscribe to:
Post Comments (Atom)

No comments:
Post a Comment