Sunday, June 15, 2008

1. Demokrasia na Tume Huru za Uchaguzi

DEMOKRASIA ilipoingia Afrika ilichukuliwa kama vile ilikuwa ni mtoto wa chama tawala na serikali iliyopo madarakani. Pengine hali iliyokuepo wakati huo [ya mzazi kukosa mkunga wa kumzalisha] ndio iliyochangia kuwa na hali kama hii.

Mwana keshapatikana, hata hivyo, je, kweli tunastahili kuendelea kama tulivyokuwa tukifanya huko nyuma au tubadilike kwa kuzingatia mahitaji ya wakati tulio nao?

Haiwezekani kamwe kuwa na Tume ya Uchaguzi inayochaguliwa na chama tawala na serikali iliyopo ambayo itaonekana kutenda haki kwa wote siku zote. Hili ni kutokana na ukweli kuwa lazima mwana amheshimu mzazi. Na ni zaidi ya hapo kwa yakini, maana hao wanaopewa nafasi hiyo wanajihesabu kama wamelishwa fadhila na huyo aliyewachagua.

Ndio maana tunapendekeza ima fa ima lazima Tume za Uchaguzi Afrika zichaguliwe kutoka kwenye watu ambao hawafungani na upande wowote wa kisiasa. Ikizingatiwa kwamba uchaguzi ndio unaotupa wabunge na wabunge ndio wanaotakiwa kuwakilisha wananchi bungeni basi kwa mantiki hiyo ni lazima vile vile yale makundi ya kijamii yanayoweza kuitwa washikadau yawe na nafasi katika kuwapendekeza wale inaoamini kuwa watasimamia uchaguzi bila kupendelea upande wowote.

Kuwa na Tume ya Uchaguzi ambayo ina huruma na huba kwa serikali iliyoko madarakani na chama tawala hakuashiria mema kwa nchi inayotaka kujenga demokrasia ya kweli na yenye amani na manufaa kwa watu wake.

Tunaamini kwamba kuwa na Tume Huru ya Uchaguzi ni mwanzo wa kuondokana na tuhuma mbalimbali zinazoambatana na uchaguzi na pia ni msingi wa demokrasia madhubuti na yenye tijara kwa wananchi wa nchi hii. Kuna nchi kadhaa Afrika kati ya zote ambazo zimeweza hili na hakuna sababu ya Tanzania kuwa namba tatu katika jambo kama hili!

Tume Huru ya Uchaguzi itakuwa inawajibika kwa wapiga kura kupitia katiba mpya tarajiwa na sheria za haki kwa mujibu wa maazimio mbalimbali ya Umoja wa Mataifa, Afrika na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na sio kiongozi au chama chochote.

Kama ilivyo kwa Tume kuwa Huru ndivyo inavyostahili pia kwa Watanzania wote kuwa huru katika kupigiwa au kupiga kura ila pale mwananchi huyo anapoamua kufanya hivyo akiwa ndani ya Chama hiki au kile cha kisiasa. Haki ya kuwa huru inastahili kuwepo wakati wote iwe kabla ya kujiunga na chama au baada ya kukiacha chama fulani.
***

No comments: