DEMOKRASIA ya kweli hufanya kazi katika nchi ambayo haina njaa; watu wake wanalipwa mishahara mizuri; na kwa ujumla hali ya uchumi hairuhusu upungufu au umasikini wa kutisha.
Demokrasia yenyewe hufanya kazi pale mtu anapolazimishwa kulinda shibe yake; kipato chake na hali yake ya uchumi kwa ujumla.
Hali kama hii haiko Tanzania. Na kwa kuwa haipo lazima wananchi wakishirikiana na wanasiasa mbalimbali kujikita katika kufikiri na kubuni shughuli mbalimbali za uchumi na kiuzalishaji mali zitakazowawezesha kwanza kutosheleza mahitaji yao ya msingi na pili kuwaweka katika nafasi nzuri ya kuimarisha uchumi na maendeleo ya nchi katika siku za baadaye.
Itakuwa ni muhali kuwa na demokrasia ya kweli pale ambapo hata mahitaji ya msingi ya watu wetu hayatoshelezwi.
Demokrasia katika hatua tuliyofikia pengine ni kuwa na mijadala inayoendelea siku zote kuona jinsi gani watu wetu watapata maji, umeme na huduma mbalimbali za jamii kiasi cha kutosheleza wote na kwa uhakika kwa maana ya kwamba teknolojia na uendeshaji vitu hivyo vyote vitakuwa ni vitu tunavyovishughulikia sisi wenyewe.
Kujitosheleza kwa maji, umeme, miundombinu, shule na vyuo, mahospitali na huduma za afya peke yake vinaweza vikawa ni shuighuli za kuingizia taifa pato la kutosha na hivyo kuharakisha kasi ya kuwatoa wananchi wetu kwenye umasikini. Lakini yote haya yanataka uwezo wa kuona mbali, kuukataa ubinafsi na kujitolea kwa viongozi kuona wananchi wao wananufaika wao kwanza kabla wao viongozi hawajanufaika. Je, tuna viongozi wa aina hii Afrika?
Umaskini huu wa kutisha aidha unaweza kuondolewa kwa kuhakikisha kuwa mikoa na sehemu za nchi husika zina uwezo wa kuendesha mambo yao ya kiuchumi na kijamii bila kuingiliwa sana na serikali kuu.
Dhana ya madaraka mikoani bado ni hai na sasa imeongezeka umuhimu wake baada ya kuona kuwa nchi zetu Afrika ni kubwa mno na hawezi mtu mmoja aliyeko huko kunakoitwa makao makuu ya nchi kuwaletea neema na ukwasi watu wa nchi nzima.
Ukweli ni kuwa mikoa ikiwa na uwezo wa kutekeleza sera zao za uchumi na kijamii kwa ushirikiano na marafiki wa ndani na nje basi nafuu na neema kwa wakazi wa mkoa husika itakuwa ni ya haraka zaidi kuliko ilivyo sasa.
Nafasi ya mikoa kujiendesha yenyewe kiuchumi na kijamii pia inalisaidia taifa kwa kuzalisha watu wanaofaa kushika nafasi za uongozi wa taifa badalal ya kuwa sisi ni watu wa kuwajaribu watu wasiotahiniwa katika tarafu hizo.
***
Sunday, June 15, 2008
Subscribe to:
Post Comments (Atom)

No comments:
Post a Comment