KILA inapokaribia uchaguzi mkuu katika nchi ya Kiafrika ndoa za haraka haraka kati ya wafanyabiashara na chama tawala, au mangimeza na chama tawala hufungwa. Matokeo ya ndoa zote hizi ni kuvunjika kila baada ya uchaguzi kwa sababu ahadi huwa siku zote nyingi kuliko uwezo wa mtawala. Na hapo ndipo nchi inapoingizwa kwenye matatizo mengine ambayo nadhani Watanzania wengi sasa watajua ninachokizungumza.
Mpaka pale kutapokuwa na uwazi kuhusu jinsi vyama vya kisiasa, yaani, chama tawala au vyama tawala na vile vya mbdala vinavyopata fedha za kujiendesha na kuendesha uchaguzi mkuu itakuwa ni kazi sana kujenga demokrasia ya kweli Afrika.
Lazima vyama vyote vya siasa viige mfano wa vyama vya SACCOS kwa kuwa na shughuli za kiuchumi na kijamii zinazoweza kuwaingizia sio tu wanachama wao bali washirika wao wengine na wao wenyewe kipato cha kutosha kujiendesha bila kujiingiza katika njia ambazo zinazoweza kuhesabika ni za kiuhalifu na za kiharamia kuliko zile za magaidi wa nje.
Ni muhimu pia kuhakikisha kuwa mawaziri, makatibu wakuu, wakuu wa mikoa, wakuu wa wilaya na viongozi wengine wa serikali hawatumii nafasi zao kufanya kazi za chama kwa kutumia fedha ya serikali. Hili sio haki na katu lisikubalike katika mwenendo wa demokrasia na uwajibikaji wa wanasiasa.
Aghalabu, hatima ya yote hayo ni kuwa ujanja huo pia huishia kuwa ujanja wa kufanya shughuli binafsi kwa kutumia mali ya umma au ya serikali.
Tumeruhusu kuwa na viongozi ambao ni wanasiasa na wakati huo ni wafanyabiashara lakini hili ni kosa. Ni lazima tulitazame upya jambo hili.
Huwezi ukawa na waziri ambaye ni mfanyabiashara na akaacha kuitumia ofisi yake kujinufaisha katika masuala binafsi. Lazima tuone hili, lazima tujue ukweli huu. Na kwamba wakati umefika wa kuamua mtu ama aolewe au kuoa biashara, au aolewe au kuoa siasa. Basi. Hakuna njia ya kati.
Hili litatuhakikishia wale wanaolipwa mshahara na serikali kuwa saa zote mawazo na moyo wao uko katika kazi waliyopangiwa na sio vinginevyo.
***
Subscribe to:
Post Comments (Atom)

No comments:
Post a Comment