NCHI iwe na demokrasia au isiwe na demokrasia lazima bunge lililochaguliwa na wananchi liwakilishe mawazo na msimamo wa wananchi wanaowakilishwa.
BUNGE linalojiegemeza pembeni ya serikali na chama chochote cha kisiasa sio bunge la watu ni bunge la wabinafsi wachache wanaotetea maslahi yao wenyewe na sio ya wale waliowatuma.
Kazi ya mbunge katika nchi yoyote inayofuata demokrasia sahihi ni kuwakilisha mawazo na masuala yanayowahusu wale waliowachagua.
Na ni wajibu wa chama chochote na serikali yoyote kuhakikisha kuwa mbunge anayefanya kazi zake za kibunge hanyimwi uhuru na haki yake hata kama hakubaliani na serikali na chama kilicho madarakani.
Ikiwa vinginevyo basi ujumbe wanaostahili kuupata wananchi ni kuwa hawana uwakilishi na sio wajibu kwao kulipa kodi kwa sababu sheria inasema pasipo uwakilishi hapana haki ya kulipa kodi.
Katika kuimarisha bunge ni dhahiri kuwa wabunge ndio wanaostahili kumchagua Kamanda Mkuu wa Polisi, Wakuu wa mikoa [kwa hali ya sasa], Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Gavana wa Benki Kuu, Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi, Jaji Mkuu na wale wengine wote ambao wanatakiwa wawajibike kwa watu na sio kwa watawala wa wakati huo.
Hatutakaa tuone mambo yanayotokea leo Zimbabwe, Kenya, Ethiopia, Zambia na Malawi hapa Tanzania.
Hili likifanyika ni kuwa Kamanda Mkuu wa Polisi atakuwa hawezi kutishwa na chama cha siasa wala mwenyekiti wake; na vivyo ndivyo itakavyokuwa pia kwa washika nyadhifa nyingine waliotajwa hapo juu.
Na pale ambapo mkuu wa polisi, mkuu wa mkoa, Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi, Jaji Mkuu na watu wengine kama hao watakuwa hawatishwi na Mkuu wa nchi au chama tawala basi itakuwa ni rahisi kwa haki kufanyika wakati wote. Na haki inapokuwepo ndipo palipo pia na ukomavu wa demokrasia.
Bunge linalokuwa ni muhuri wa serikali iliyoko madarakani na na chama tawala basi inakuwa ni hasara kwa kizazi cha sasa na kizazi kijacho.
Ni ujasiri kwa mbunge yeyote wa leo kusimama, kutetea na kupigania haki hii kwa faida ya kizazi cha leo na kizazi cha kesho.
***
Sunday, June 15, 2008
Subscribe to:
Post Comments (Atom)

No comments:
Post a Comment