Tafsiri ya Tume Huru ya Uchaguzi
TUME Huru ya Uchaguzi ni kamati yenye nguvu za kisheria inayoundwa na wananchi walio huru na wasioshawishiwa na mahakama, bunnge, serikali au chama chochote cha kisiasa katika utendaji wa kazi zake. Katika demokrasia makini wajumbe wa Tume Huru hutokana na makundi mbalimbali katika jamii bila kujali kwamba wana elimu ya sheria au la. Wanaostahili kuwa wasomi wa sheria sio wajumbe wa Tume bali watumishi wa Tume. Watumishi hawa huwajibika kutoa ushauri wa kisheria katika maamuzi yote yanayofanwa na Tume ili kuhakikisha wakati wote Katiba ya nchi na sheria zake zinazingatiwa na kuheshimiwa.
Tume yoyote ya Uchaguzi inayoundwa na kubarikiwa na Mwenyekiti wa Chama fulani au Rais wa nchi aliyepo na inayotokana aghalabu na watu waliopewa kabla ya hapo nyadhifa za chini na kiongozi huyo huyo haiyumkiniki kuwa huru kwa sababu mbili kuu. Kwanza, watu hao huwa na mtazamo na msimamo uleule wa seriali au chama kilichowateua. Pili hujikuta wana wasiwasi na nafasi zao na ili kuzilinda inabidi wajipendekeze kwa viongozi walioko madarakani, aghalabu huwa ni tatizo kubwa wakati wa kuhesabu na kutangaza kura kwa sababu hutaka kuwasaidia wale waliowalisha fadhili ya kuwa wajumbe wa Tume ya Uchaguzi.
Kufuatia kukubalika kwa mfumo wa Vyama Vingi baadaye zilipitishwa sheria mbalimbali zilizochangia au kukwaza maendeleo ya mfumo wa vyama vingi nchini. Sheria hizo ni pamoja na zile zinazosimamia uanzishwaji, uendelezaji na uboreshaji wa siasa za mfumo wa vyama vingi.
Kwa upande mmoja kanuni za demokrasia zinazokubalika kimataifa zimechangia kuchipuka kwa maendeleo ya mfumo wa vyama vingi hapa nchini. Kwa upande mwingine, sheria zetu zenyewe zilizotungwa chini ya mfumo wa chama kimoja zimekuwa ni kikwazo hapa na pale katika uendelezwaji na uimarishwaji demokrasia nchini.
Kwa kuwa Tume Huru zilizopo zilianzishwa katika mazingira ya Chama kimoja wanaharakati wa demokrasia wanaoona kuna mapungufu kadhaa yanayochangia kudumaa kwa demokrasia nchini.
Tume huru huzaliwa na Katriba mpya sio katiba yqa viraka
Ili tume hizo kuwa na mashiko taibu na halali ya kikatiba na kisheria ilipaswa kwanza kwa serikali ya Muungano na ile ya Zanzibar pengine na ya Tanganyika kuwa na katiba mpya. Hili halikufanyika.
Katiba mpya inahitajika ili kujenga mazingira ya haki na usawa kati ya vyama vyote vya siasa na wanasiasa. Haiwezekani kwa chama kimoja kuendelea kutumia fursa za upendeleo zilizopo katika katiba mapokeo bila kusababisha misuguano isiyokwisha katika mahusiano ya vyama na jamii kwa ujumla.
Chini ya chama kimoja jengo lilikuwa halina ghorofa. Baada ya kuja kwa mfumo wa vyama vingi sasa jengo linahitajika kuwa na ghorofa mbili kama sio tatu. Je, kweli tutaweza jenga maghorofa haya kwa kutumia msingi au katiba iliyopo?
Chama tawala kwa kwa kung'ang'ania katiba ya zamani ni sawa na kutaka kuwauzia wengine ghorofa lote. Lakini pale wengine wanapokataa sasa inadai itavunja sakafu ya chni na wao washikilie ghorofa zao huko juu kwa juu. Huu ni Uabunuwasi mtupu na jambo lisilokubalika.
Marekebisho katika sheria ya Tume Huru yamekuwa yakifanyika kwa mfumo wa viraka kama vile inavyofanyika kwa Katiba ya Jamhuri ya Muungano iliyopo leo.
Wanaodai hatuhitaji mabadiliko ya Kikatiba hawana hoja za maana zaidi ya kusema kwamba ile iliyopo bado inawafaa Watanzania.
Wanatumia zaidi hoja ya nguvu na sio nguvu ya hoja. Ili mradi chama chao kiko madarakani na katiba iliyopo inawalinda wao zaidi basi wanadhani kwamba hatuhitaji katiba mpya. Ni pale watakapojikuta upande wa pili ndipo watakapotambua tu umuhimu wa kuwepo kwa katiba mpya.
Swali la kujiuliza hapa ni je, katiba iliyotungwa wakati wa mfumo wa Chama Kimoja na katika mfumo wa siasa wa Kijamaa, kweli inaweza kukidhi mahitaji ya mfumo wa Vyama Vingi, Siasa za Ushindani na Soko Huria kwa mapana na marefu yake kikamilifu?
Kwanini Tume Huru ?
Jibu hapa linaweza kupatikana kwa kuangalia masuala mbalimbali ya kisiasa, kiuchumi, kijamii, kiteknolojia, kiutamaduni na kiutandawazi yanayolilia kila kukichwa mabadiliko ya msingi ili maeneo haya yaweze kufanya kazi zake barabara.
Ikumbukwe kwamba demokrasia kama mfumo wa siasa unaathiri na unaathiriwa na masuala mbalimbali yanayowahusu au kuwazunguka watu na nchi husika.
Mathalani, kasi ya maendeleo ya kiuchumi, kiteknolojia na kijamii huathiriwa na kuwepo au kutokuwepo demokrasia pana na ya kina. Uwezo wa watu kuchangia maendeleo ya nchi yao kwa njia hii au ile vile huathrika na kuwepo au kutokuwepo kwa demokrasia. Kwa maneno mengine, kuwepo kwa demokrasia kunaruhusu maingiliano na mahusiano mbalimbali katika jamii yanayochangia maendeleo ya kiuchumi na kijamii kwenye nchi husika. Kutokuwepo kwa demokrasia kunazuia maingiliano na mahusiano haya na hivyo kudumaza nchi kimaendeleo.
Funguo na kofuli la kupanuka au kusinyaa kwa demokrasia kwa kawaida vinashikiliwa na Tume Huru. Kama Tume kweli ni Tume Huru kazi ya kukua na kupanuka kwa demokrasia inakuwa rahisi mno. Kama Tume sio huru kukua kwa demokrasia sio tu kinakuwa kitu cha polepole sana bali pia huweza kabisa kusimama na kusinyaa.
Hali ilivyo hivi sasa ni kuwa Chama Tawala kina haki zaidi katika kuamua Mwenyekiti wa Tume awe nani na wajumbe wa Timu hizo wawe nani.
Sasa hebu fikiria pale ambapo Timu ya Simba inapokuwa na ruhusa ya kumchagua Refa wa mechi kati yao na Yanga. Na wasiishie hapo tu, bali pia Simba wapewe ruhusa ya kuchagua nani wacheze katika timu ya Yanga na marefa wasaidizi na kamishna wa mechi awe nani. Yanga itakwenda uwanjani kweli?
Swali kubwa zaidi hapa ni je, Wajumbe wa Tume Huru ya Uchaguzi wanatakiwa wamwakilishe nani? Rais aliyeko madarakani? Chama kilichoko madarakani ? Serikali iliyopo ? Wananchi ? Au wafadhili ?
Ukweli ni kuwa wajumbe wa Tume Huru wanatakiwa kutoka kwenye makundi mbalimbali ya wanajamii yasiyofungamana na upande wowote kisiasa.
Makundi haya kwa kuyagawa katika mafungu makubwa kitarafu yanajumuisha wafanyakazi wa umma, wafanyakazi sekta binafsi, wanaojiajiri, wakulima, wafanyabiashara, wafugaji, wawindaji, wavuvi, wanafunzi na wasiosoma.
Ukigawa kijinsia yana wanawake, wanaume, vijana na watoto. Ukiyagawa kiumri kuna watoto, vijana, watu wazima na wazee. Ni muhimu kuyaangalia makundi haya na kuona ni namna gani yanaweza kuchangia uwakilishi katika Tume Huru.
Wawakilishi katika Tume Huru ya Uchaguzi ndio wanaoamua kama makundi hayo yataishi kwa amani na neema au la baada ya kila uchaguzi kufanyika. Na kazi yao hiyo huweza kuharibiwa katika hatua yoyote ile ya mchakato mzima wa uchaguzi mkuu iwe ni katika maandalizi, kuandikisha wapigaji kura, upigwaji kura au kuhesabiwa kwa kura na hatimaye kutangazwa matokeo.
Hili linaonesha uzito wa dhamana waliyo nayo wajumbe na viongozi wa Tume huru. Kutokana na hili panahitajika umakini mkubwa katika kuwachagua wajumbe hao. Na hii haiwezi kuwa kazi ya serikali iliyopo madarakani au chama tawala peke yake. Maana kama kawaida tabia ya mwamba ngoma ni kuvutia ngozi upande wake.
Umuhimu wa wajumbe huru na makini
Kushirikishwa na kuwepo kwa watu makini katika Tume Huru ya Uchaguzi ndio hatua ya mwanzo na ya mwisho katika kujenga demokrasia ya kweli katika nchi.
Kwa mantiki hii ninapendekeza kwamba kabla ya kuwachagua wabunge na Rais pengine tunastahili kuwa na Uchaguzi wa Wajumbe wa Tume Huru ya Uchaguzi.
Uchaguzi wa Wajumbe wa Tume Huru, hata hivyo, hautafanyika kila baada ya miaka mitano. Wajumbe hao wakishachaguliwa na kukubalika na wananchi wataendelea kuwepo kwenye Tume hadi kufa kwao au kuondolewa mmoja mmoja au wote pindi wananchi wanapoonesha kukosa imani na mmoja wao au Tume nzima.
Kwa mantiki hii, tutakuwa na Wajumebe wa Tume Huru ya Uchaguzi wanaochaguliwa na wananchi kwa upande mmoja na kwa upande mwingine Rais na wabunge wanaochaguliwa na wananchi. Kwa hiyo hakutakuwa na kumwogopa au kumwabudu mwenzie kama ilivyo hivi sasa. Sio lazima wajumbe hao wawe majaji au wanasheria. La muhimu hapa ni utu, uadilifu na uhuru wa mtu. Izingatiwe kuwa majaji na wanasheria wataingia kama wafanyakazi wengine katika sehemu wanaokstahili kuwepo. Nayo sio nyingine bali katika meza za kutoa ushauri wa kisheria kwa wajumbe.
Tume Huru itawajibika kwa wananchi. Wakati wowote wananchi wanapokosa imani nayo uchaguzi mwingine utaitishwa na hivyo kuwatoa wasiofaa na kuwarejesha wa zamanai au kuwaingiza wapya wanaonekana kuwa wanafaa.
Mapungugu mbalimbali kushughulikiwa
Sheria iliyounda Tume Huru ya Uchaguzi imeanisha kazi kadhaa zinazopaswa kufanywa na Tume. Hata hivyo, pana mapungufu kadhaa ambayo bado yanaweza kushughulikiwa na kurekebishwa mara kwa mara ili hatima ya yote baada ya miaka michache kuwe na sheria, kanuni na taratibu ambazo sio rahisi kukoselewa na hivyo kutoa fursa ya kuchipuka sio tu kwa Tume Huru bali kwa taasisi nyingine za kidemokrasia ambazo ni huru kivitendo na endelevu.
Ni lazima pia Tume Huru ya Uchaguzi iwe na Ruiya au Visheni. Katika nchi nyingi za Kiafrika hii itakuwa ni: ' Kuona Nchi inakuwa na demokrasia pana na ya kina hadi Vijijini.
Azma au Misheni inaweza ikawa ni kufanya yale yote yanayosaidia kujenga na kuwepo kwa demokrasia halisi nchini.
Baada ya hapo Tume inaweza ikaweka mikakati, mbinu, kanuni, mipango na taratibu mbalimbali ya kujenga na kuendeleza demokrasia nchini.
Masharti ya Awali ya Uchaguzi huru
Wakati wa Uchaguzi Tume itatakiwa kuhakisha kuwepo:
i. Haki katika upigaji na ufuatiliaji zoezi la kupiga kura
ii. Usawa katika upigaji na ufuatiliaji zoezi la kupiga kura
iii. Uwazi katika upigaji na ufuatiliaji zoezi la kupiga kura
iv. Ukweli katika upigaji na ufuatiliaji zoezi la kupiga kura,
v. Hali isiyo ya vitisho, uonevu, upendeleo au unyanyaswaji katika upigaji na ufuatiliaji zoezi la kupiga kura
vi. Umakini na uwajibikaji katika upigaji na ufuatiliaji zoezi la kupiga kura.
Haya yakiangaliwa kwa makini basi wakati wa Uchaguzi wananchi watakuwa na imani na Tume. Yasipokuwepo ni wachache sana watakaokuwa na imani na Tume na wasimamizi wake. Aghalabu kukosekana kwa hayo hapo juu ndio unaokuwa mwanzo wa kutofautiana, kuhitilafiana na kugombana. Hali ambayohatimaye hufuatiliwa na nchi kutokuwa na amani na mshikamano.
Nikamilishe sura hii kwa kukumbushwa kwamba kuwepo kwa Tume Huru ya Uchaguzi ambayo imechaguliwa na wananchi wenyewe na isiyoyumbishwa na mtu yeyote au chama chochote cha siasa au serikali au vyombo vya dola ndio mwanzo wa demokrasia kuchipuka na kukua katika nchi zetu za Kiafrika.
Copyright © 2009 S.W.I.Makilla
Friday, June 5, 2009
Subscribe to:
Post Comments (Atom)

No comments:
Post a Comment