Tuesday, December 28, 2010

Ujinga Kuhusu Katiba Usivumiliwe

Nikiwasikiliza wakuu wa vyombo vya dola ninahsi kwamba hawaijui katiba, tena katika sehemu muhimu zinazowahusu, na hasa katika kuendesha kazi zao kwa haki na usawa kati ya wananchi. Ninapozungumza wananchi hapa ni kuwa hata rais na watumishi wa serikali ikiwemo polisi na wanajeshi ni wananchi kama ilivyo wanasiasa mbalimbali na raia kwa ujumla wao. Hakuna kati yetu anayestahili kuwa juu ya katiba au sheria. Lakini pamekuwa na mchezo kwa muda mrefu wa chama fulani cha kisiasa kule makao makuu na hata ngazi za chini katika ofisi za mikoa, wilaya na matawini kujiona kwamba wao wako juu ya katiba ya nchi na sheria. Huu ni mchezo tunaotaka uishe kwa kuwa na katiba mpya. Haukubaliki. Na wananchi watakuwa wajinga kuukubali. Enzi za udikteta wa chama kimoja umekwisha na tusikubali urudi maana yanayotokea katika baadhi ya nchi za kijamaa kwa ile iliyokuwa Russia leo yanatisha na iwe fundisho kwetu kukataa kata kata kuruhusu mizizi ya udikteta wa mtu au chama kuanza tena kuota hapa nchini.

Kosa kubwa nchi za Kiafrika zilizofanya ni lile la kuwaabudu viongozi wao na kuwafanya mungu wadogo hapa duniani. Na hakuna asiyependa kuabudiwa kama ilivyo kawaida yetu viumbe. Lakini hili si tu kosa la kiimani ni kosa katika maisha yetu ya kila siku kwa sababu watu hao wanaoabudiwa wakiwa wajinga au kuleweshwa na cheo na madaraka watataka hata kumzidi Mungu. Na kisha wanaowafuatia nao watataka kuwa miungu wadogo pia kama tunayoyaona yakitokea huko Kigoma, Arusha, Mwanza, Mara na kwingineko ambako Mungu wetu wa kisiasa wakubwa kwa wadogo hawataki upinzani ufurukute na kuwafanyia wananchi wao yaliyo mema, ya haki na wajibu kwa upande wao.

Maandamano na kuandamana hakuvunji katiba na sheria. Ni sehemu ya katiba na sheria. Na wanaovunja amani na mshikamano nchini sio wengine ila wale wanaotumiwa (na hawajui katiba na sheria kwa ukamilifu wake) na baadhi ya wanasiasa kuingilia haki ya kikatiba ya wananchi wengine.

Tuna kazi kubwa ya kuwaelewesha askari wetu kuwa bosi wao ni mwananchi na sio chama chochote cha siasa au ofisi ya mkubwa fulani serikalini. Na aliye na haki baina yetu juu ya suala hili la mahakama ni idara ya sheria/mahakama iliyo huru ambayo kwa sasa ni sawa na haipo.

Katiba yetu iko wazi kabisa katika suala la maandamano. Maandamano ni haki ya mwananchi. Kinachotakiwa ni kwa polisi, mgambo au wateuliwa wa chama au kundi husika watakaohakikisha usalama na amani wakati wa maandamano hayo. Lakini bado hii inabaki nikazi ya polisi, na haki ya kikatiba ya kila Mtanzania kuandamana ili mradi wanaofanya hivyo wanathibititha kutovunjwa imani. Polisi au FFU wanatuchekesha wanaposema walihisi 'uvunjikaji' wa amani endapo maandamano yatafanyika.

Soma Kifungu cha katiba kifutacho kwa uhakika wa hili : Katiba kifungu namba " 20.-(1) Kila mtu anastahili kuwa huru, bila ya kuathiri sheria
za nchi, kukutana na watu wengine kwa hiari yake na kwa amani,
kuchanganyika na kushirikiana na watu wengine, kutoa mawazo
hadharani, na hasa zaidi kuanzisha au kujiunga na vyama au
mashirika yaliyoanzishwa kwa madhumuni ya kuhifadhi au
kuendeleza imani au maslahi yake au maslahi mengineyo."

Kifungu hiki ni sehemu ya sheria za nchi wananchi walioziwekea wenyewe katika katiba ambayo leo baadhi yetu hatuitaki kwa sababu ya mapungufu yake ikiwemo kutafsiriwa ndivyo sivyo na vyombo vya dola.


Kama ilivyo katika jambo lolote ambalo hatimaye linaanza kukubalika na umma na nguvu ya umma kuanza kuliendesha lazima pazuke kambi mbili kuu.

Kambi ya kwanza ni ile ya lambalamba (sycophants) ambao hawana sababu nyingine ya kupinga kuwepo kwa katiba mpya ila tu kujihakikishia kuendelea kuwepo kwao leo na kesho. Hao hucheza karata eti umma utashindwa na mabavu ya kidikteta yataendelea kuwepo. Lakini sote tunajua kuwa udikteta sikuzote siku zake zinahesabika. Maana hili sio jambo linalokubalika na wananchi. Wananchi hutaka kujiendeshea mambo yao bila ya kufuatwa fuatwa na kusagwasagwa ili waridhie upande huu au ule. Umma unachokitaka na hoja thabiti za kuelewa bora na kinachowafaa kinyume na uongo, udhaifu na kisichowafaa.

Na kambi ya pili ni ile ya wale wana vukuto, wanaharakati na wafunguka macho wanaodai haki ambazo ziko wazi ndani ya katiba ya nchi.

Ni jambo la kusikitisha kwamba wakati nchi yetu ina maeneo ambayo majambazi wanavamia na kukata kata mapanga abiria eti FFU wako Dar es salaama kupambana na maandamano ya CUF na hatari yake ni kwa kuwa sio chama tawala tu na sio vinginevyo; wakati wanachi katika asilimia 70 ya hospitali zetu wilayani hawana magari ya wagonjwa tuna magari ya kuwamwagiwa watu maji ya pilipili yanayowasha; wakati tunahitaji zana na vifaa vya kutuondoa kwenye umaskini tunanunua na kutumia mabomu ya kuwalalzimisha watu kulia. Ama hakika aliyelewa na madaraka ni mwepesi wa kukufuru na kufanya isirafu ilhali anaona kila kitu kwake ni sawa!

No comments: